Home » » ASKOFU:ALAUMIWE JK,SI WARIOBA

ASKOFU:ALAUMIWE JK,SI WARIOBA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
UMOJA wa Makanisa ya Kikristo mjini Dodoma, umekemea baadhi ya viongozi wa serikali na wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kumbeza aliyekuwa Mwenyekiti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji mstaafu, Joseph Warioba. 
Akiwasilisha tamko hilo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Makanisa ya Kikristo, Askofu, Dk. Elia Mauza, alisema anayepaswa kulaumiwa si Jaji Warioba bali Rais Jakaya Kikwete aliyemuamini na kumteua. 
Alisema mwelekeo wa Bunge hilo unayumbishwa na wana siasa wanaojali masilahi yao.
 “Kimsingi wanasiasa wanatupeleka pabaya,  sisi Umoja wa Makanisa ya Kikristo mjini hapa tunatoa tamko la kulaani mwenendo wa Bunge hilo hasa kwa kumkejeli Jaji Warioba.
“Jaji Warioba na tume yake wamefanya kazi kubwa, hatuoni sababu ya yeye kudhalilishwa kwa kumshambulia kwa maneno mengi, kama kuna sababu ya kutoa lawama basi alaumiwe Rais Kikwete.
“Kikwete ndiye aliyeunda tume ya katiba na wakati akipokea rasimu ya kwanza na ya pili aliisifia kwamba ni nzuri sana na aliipongeza tume hiyo, je, kama kulikuwa na upungufu kwanini hakumkosoa tangu mwanzo ili aurekebishe kabla ya kuutoa kwa Watanzania?” alihoji Dk. Mauza.
 Dk. Mauza alisema ni fedheha kwa Bunge Maalumu kuacha kujadili mchakato wa Katiba na kuelekeza mashambulizi kwa Jaji Warioba na tume yake.
 “Katiba si mali ya wanasiasa wala chama chochote cha siasa, katiba ni mali ya wananchi na kinachotakiwa kujadiliwa na kuboreshwa ni kile kilichopo ndani ya rasimu kwani hayo ndiyo mawazo ya Watanzania.
 “Nasema katiba si mali ya wajumbe zaidi ya 600, bali ni ya Watanzania zaidi ya milioni 45, hivyo watu wachache kukaa ndani ya Bunge badala ya kujadili  mambo ya kwenye rasimu na kuanza kujadili mambo yao ni aibu kwa taifa,” alisema Askofu Dk. Mauza.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa