Home » » HATA ZIUNDWE TUME 100,ZITATUHUMIWA KUCHAKACHUA TAKWIMU

HATA ZIUNDWE TUME 100,ZITATUHUMIWA KUCHAKACHUA TAKWIMU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Kuna tuhuma nzito kuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilichakachua takwimu za maoni ya wananchi ili tu kukidhi hoja ya muundo wa Serikali tatu.
Ndiyo maana baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wanamnyooshea kidole moja kwa moja aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Joseph Warioba na wengine wakiilaumu tume kwa jumla wake.
Binafsi, sielewi msingi wa shutuma hizi kuelekezwa moja kwa moja kwa Jaji Warioba ama Tume, wakati ilikuwa na watumishi wa umma waandamizi ambao nao walishirikishwa katika Tume hii.
Hata Machi mwaka huu wakati akiwasilisha bungeni Rasimu ya Katiba, Jaji Warioba alisema juu ya uwepo wa watumishi hawa ambao kimsingi, ndio waliochambua na kuchakata maoni ya wananchi.
Jaji Warioba alisema: “Namshukuru Rais kwa kuipatia Tume watumishi wa Sekretarieti walio makini, wenye ujuzi, utaalamu na uelewa katika fani zao waliowezesha kukamilisha kazi yake kwa ufanisi.”
Ni watumishi hao ambao walimfanya Jaji Warioba na wenzake kusimama kifua mbele na kutoa takwimu za wananchi waliotoa maoni yao Tanzania Bara na Zanzibar waliotaka Serikali tatu.
Kwa mujibu wa Jaji Warioba, kati ya waliotoa maoni yao kwa upande wa Zanzibar, asilimia 34 walitaka Serikali mbili, asilimia 60 Serikali ya mkataba na asilimia 0.1 walipendekeza Serikali moja.
Halikadhalika kwa upande wa Tanzania Bara, asilimia 13 ya waliotoa maoni walitaka Serikali moja, asilimia 24 wakapendekeza muundo wa Serikali mbili na asilimia 60 wakataka Serikali tatu.
Mbali na wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutilia shaka takwimu hizo, hata Rais Kikwete mwenyewe, aliyeiteua Tume hii haiamini.
Akihutubia Bunge Machi 21,2014, Rais Kikwete anasema: “Wanasema pia kwamba mbona taarifa ya Tume yenyewe ukurasa wa 66 na 67 inaonyesha watu waliotoa maoni juu ya muungano ni 47,820”
“Kati ya hao ni watu 17,280 sawa na asilimia 37.2 ndio waliotaka Serikali tatu, asilimia 29.8 walitaka Serikali mbili, asilimia 29.8 wakataka Serikali ya mkataba na asilimia 7.7 wakataka Serikali moja.”
Rais akahoji swali ambalo limekuwa ndiyo msingi wa hoja za wajumbe wengi wa Bunge Maalumu la Katiba wanaotoka CCM. Aliuliza: “Hii hoja ya Watanzania wengi kutaka Serikali tatu msingi wake upi?”
Mbali na Rais Kikwete, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Benard Membe naye akaleta hoja kuwa Tume ya Jaji Warioba italaaniwa kwa kuleta pendekezo la Serikali tatu.
Miongoni mwa wajumbe wa Tume hii wanaotuhumiwa kuchakachua takwimu ni watu walioitumikia nchi kwa uadilifu mkubwa tena wengine wakiwa ni wateule wa Rais.
Jaji Warioba aliwahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jaji Agustino Ramadhan aliwahi kuwa Jaji Mkuu wa Tanzania. Wote hawa hatuwaamini?
Katika kuilaumu Tume ya Jaji Warioba, si Rais Kikwete, mawaziri wake wala wajumbe wa Bunge Maalumu wanaogusa uwepo wa watumishi waandamizi wa Serikali ndani ya Tume hiyo.
Kama hata Rais hana imani na watumishi hawa waandamizi wa Serikali walioisaidia Tume kuchambua takwimu, kwa nini hawafukuzi kazi au kuwawajibisha kwa kukiuka maadili ya Utumishi wa Umma?
Nauliza swali hili kwa sababu, tumeelezwa Tume hii ilitumia karibu Sh70 bilioni za walipa kodi masikini wa Tanzania. Kama ni kweli takwimu zina kasoro, Rais anasubiri nini kuwawajibisha?
Hebu tuamini kwamba takwimu hizo zimepikwa ili kuhalalisha tu muundo wa Serikali tatu, tujiulize na Tume nyingine zote zilizowahi kuja na mapendekezo ya muundo huo huo nazo zilipika takwimu?
Sasa kama takwimu hizi si sahihi, kwanini Rais asitumie mamlaka yake akalivunja Bunge Maalumu la Katiba na kuunda Tume nyingine kukusanya maoni? Kuna maswali mengi kuliko majibu.
Kinachoonekana hapa, Serikali ya CCM haina dhamira ya dhati ya kuwaletea Watanzania katiba bora kwa vile mapendekezo ya Serikali tatu hayaletwa leo wala jana. Ni wimbo usiopendwa na wakubwa.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa