Home » » ISINGEKUWA SHERIA HII,MAMBO YANGEVURUGIKA BUNGE LA KATIBA

ISINGEKUWA SHERIA HII,MAMBO YANGEVURUGIKA BUNGE LA KATIBA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, ibara ya 26 kifungu kidogo cha pili kwa sasa inatajwa kuwa kikwazo kikubwa kilichowekwa kwa kundi lenye wafuasi wengi kuamua kila kitu bungeni.
Sheria hii inasema: Ili Katiba inayopendekezwa iweze kupitishwa katika Bunge, itahitaji kuungwa mkono kwa wingi wa theluthi mbili ya idadi ya wajumbe wote wa Bunge kutoka Tanzania Bara na Tanzania Zanzibar.
Sheria hii inaungwa mkono na Kanuni za Bunge hilo, ibara ya 64(1) ambayo inasema mambo yanayojadiliwa na kamati yataamuliwa kwa kuungwa mkono na theluthi mbili ya wajumbe wote wa Kamati kutoka Tanzania Bara na theluthi mbili ya wajumbe wote wa kamati kutoka Tanzania Zanzibar.
Kanuni hiyo, inaendelea kufafanua kuwa, isipokuwa uamuzi hata kama haukufikia theluthi mbili, suala hilo litapelekwa kwenye Bunge Maalumu.
Kwa sasa sheria na kanuni hii, inaonekana ndiyo itarejesha m mwafaka na maridhiano kwa kila kundi kama kweli kuna nia ya dhati ya kupatikana Katiba Mpya.
Mjumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, Kajubi Mkanjanga anasema sheria hii, kwa sasa ndiyo ambayo inazuia kutungwa katiba ya chama kimoja au kikundi cha watu wachache.
Anasema Msingi wa Sheria hii ni kuweka utaratibu utakaowezesha kujenga mwafaka wa kitaifa katika masuala yenye masilahi kwa taifa.
“Sheria hii inarejesha mazungumzo ya pande zinazokinzana, inarejeha kuondoa dharau baina ya makundi na kulazimisha maridhiano katika kupata Katiba Mpya” anasema Mkajanga
Sheria ilivyowakaanga wajumbe
Ukali wa sheria hii, ulianza kubainika katika zoezi la kura katika kamati zilipokuwa zinapitisha ibara mbali mbali. Katika sura ya kwanza na sura ya sita. Katika zoezi hilo, kamati 10 kati ya 12 za Bunge Maalumu la Katiba, zilishindwa kupata theluthi mbili katika kufanya mabadiliko ya ibara katika sura hizo ya kwanza na sita hasa zile ambazo zilikuwa zinafumua Rasimu ya Katiba. Wajumbe wa Zanzibar ndiyo ambao kwa kiasi kikubwa, walikwamisha upatikanaji theluthi mbili.
Sura ya kwanza ya Rasimu, ilikuwa inazungumzia Jina, Mipaka, Alama, Lugha na Tunu za Taifa na Sura ya Sita, inazungumzia Muundo wa Jamhuri ya Muungano
Kamati mbili ambazo zimeweza kupata theluthi mbili katika kufikia uamuzi ya kutengua baadhi ya vifungu hasa juu ya Muundo wa Muungano ni kamati zilizokuwa zinaongozwa na Hamad Rashid na Kamati ya Kidawa Hamis na kamati ya Dk Fransis Michael.
Ngeleja atamba kupata theluthi mbili
William Ngeleja ni Makamu Mwenyekiti wa kamati namba tisa, anasema kupata theluthi mbili, katika kufikia uamuzi ya Serikali mbili kunawezeka.
Mjumbe huyo, anasema kama kwenye kamati yake wameweza kupata theluthi mbili za Zanzibar na Bara, haoni ni kwa nini ikosekane bungeni.
“Kama sisi katika sura ya kwanza na sita, tumepata theluthi mbili, ina maana inawezekana kabisa bungeni kuzipata na hivyo kuendelea na mfumo wa serikali mbili ambao unaungwa mkono na Watanzania wengi” anasema Ngeleja. Bunge la Jamhuri lina wajumbe 628, wajumbe kutoka Zanzibar ni 212 sawa na asilimia 33.8% na wajumbe kutoka bara ni 416 sawa na asiliami 66.2% ya wabunge wote.
Mwenyekiti wa kamati namba tano, Hamad Rashid, pia alieleza kamati yake, kuweza kupata theluthi mbili za Bara na Zanzibar katika kufikia uamuzi.
Anasema kwa maana hiyo, kamati yake itabadili vifungu kwenye rasimu ambayo vinaeleza muundo wa Serikali tatu katika sura ya kwanza na ya sita.
Ibara zilizopata ugumu kupata theluthi mbili
Katika sura ya kwanza ibara ya kwanza kifungu cha kwanza. kilichokosa theluthi mbili kinasomeka kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni nchi na Shirikisho lenye mamlaka kamili ambalo linatokana na Muungano wa nchi mbili Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Akizungumza na gazeti hili, Mwenyekiti wa kamati namba sita, Stephen Wasira anasema katika kamati yake, ibara hiyo, imeshindwa kupata theluthi mbili, ili kuweza kufanyiwa marekebisho. “Kwa upande wa bara tulipata theluthi mbili lakini Zanzibar imekosekana na tumeacha kama ilivyo kwani matokeo haya ya kamati siyo mwisho”anasema Wasira.
Alisema hata katika sura ya 6 ibara ya 60(1) ambayo inasema Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakuwa ni ya muundo wa Shirikisho lenye Serikali tatu, ambazo ni serikali ya Jamhuri ya Muungano, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Tanganyika theluthi mbili ya Zanzibar ili kutengua kifungu hicho imeshindwa kupatikana.
“Lakini huu siyo mwisho kama nilivyosema awali. Tukirudi bungeni tutapiga kura kwa wajumbe wote na ndiyo itakuwa na uamuzi wa mwisho kama Muundo wa Muungano utakuwa na serikali tatu ama mbili ambao utapelekwa kwa wananchi” anasema Wasira
Vifungu hivi pia kwa mujibu wa wenyeviti wa kamati nyingine, isipokuwa kamati moja tu ya Tano, ambayo inaongozwa na Hamad Rashid, havikupata kura theluthi mbili na hivyo kubaki kama vilivyo kwenye rasimu. ,
Ukawa: Sheria ya theluthi mbili imewaokoa
Wanasheria wawili, kutoka wajumbe wa kundi la Katiba ya Wananchi, Tundu Lissu na Ismail Jusa, wanasema sheria hiyo, sasa ndiyo mwamuzi wa wa mwisho. Ndiyo, ambayo inaonesha siyo rahisi CCM kuliburuza Bunge hilo kama ambavyo walitegemea.
Jussa anasema sura ya kwanza na ya sita ndiyo kiini ya rasimu hivyo, kama vikikosa theluthi mbili ya kutenguliwa kwa kiasi kikubwa rasimu itabaki kama ilivyo.
“Tumeanza na sura ambazo ni uti wa mgongo wa Katiba kwa sababu huwezi kuandika katiba kama hujajua mfumo wa nchi unakwendaje,”anasema.
Alisema kwa taarifa alizo nazo katika kamati zote, CCM wamekuwa na mapendekezo yao kwa kila ibara ambayo wanataka yaingizwe katika Rasimu ya Katiba lakini sasa wanakwama.
Alisema pasipokuwa na Katiba iliyopendekezwa na wananchi kutaleta mpasuko mkubwa ndani ya nchi.
Jussa alisema kwa sasa ili kuhakikisha kuwa na msimamo mmoja, wajumbe wa upinzani na makundi yanayounga mkono Muundo wa Serikali tatu, kutoka Zanzibar watakuwa wakipiga kura ya wazi.
Lissu akizungumzia matokeo ya awali, anasema kwa sasa CCM ndiyo inaweza kuanza mkakati wa kuvuruga Bunge kwani tayari wamejua hawana theluthi mbili ya Zanzibar ili kubadili rasimu kama wanavyotaka.
Je, Sheria hii inaweza kuzuia Bunge kupitisha serikali mbili katika vikao vinavyoendelea? Tusubiri.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa