Home » » OLUOCH ASEMA HAKUKIMBIA BUNGENI

OLUOCH ASEMA HAKUKIMBIA BUNGENI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Ezekiel Oluoch, Naibu Katibu Mkuu Chama cha Walimu (CWT)
 
Mjumbe  wa Bunge Maalum la Katiba, Ezekiel Olouch, ameliambia bunge kuwa hakususia kiako Jumatano iliyopita, bali alipata ruhusu kutoka kwa  mwenyekiti wa bunge hilo, Samuel Sitta.
 Oluoch alitoa kauli hiyo jana bungeni baada ya kupokea taarifa mbalimbali zikimwambia kuwa amekimbia bungeni sambamba na wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

 Wajumbe hao waliondoka bungeni wakidai pamoja na mambo mbalimbali, bunge hilo linaendeshwa kwa ubaguzi, vitisho na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kina rasimu yake mbadala.

Alisema watu mbalimbali walimtumia meseji wengine walimpigia simu wakimuuliza kwa nini hawamuoni kwenye kiti chake huku wengine wakitaka kujua kama na yeye alitoka nje.

"Mheshimiwa Mwenyekiti, utakumbuka kuwa siku ya Jumatatu nilikuandikia kinoti kwamba naomba nichangie siku ya Jumanne au Jumatano asubuhi ili mchana niweze kuondoka Dar es Salaam kwa ruhusa yako,” alisema na kuongeza:

“Na ukafanya hivyo, ukanipanga kuchangia siku ya Jumanne na Jumatano asubuhi nilihudhuria kikao cha bunge kama kawaida…na mezani kwako nikaomba ruhusa, kama ambavyo nimekuwa nikifanya ninapoondoka katika jengo hili,”

 “Katika  meza yako, ruhusa yangu inaonyesha kuwa nitarudi siku ya Jumatatu jioni na ndivyo nilivyofanya na kwa kuwa nimetekeleza matakwa ya kanuni, mimi sikuwa nimetoka wakati watu wa Ukawa walipotoka,” alisema.

Kwa mujibu wa Oluoch,  ataendelea kuwepo ndani ya bunge hilo hadi mwisho na kuwa hausiki na kundi lolote la Ukawa wala la Tanzania Kwanza.

“Na watu wote hapa wanajua kwamba sijawahi kuhudhuria katika kikao chochote cha Ukawa wala Tanzania Kwanza, na wenzangu wanaohudhuria kutoka kundi la 201 wapo hapa hawajawahi kuniona.

“Lakini Mheshimiwa mwenyekiti, napenda kusema kwa kuwa jina langu ni tamu ndani ya Bunge hili, nisipoonekana watu wote wanajua Oluoch hayupo…nawahakikishia kwamba nimerudi, kuwawakilisha walimu katika bunge hili,” alisema.

Katika hatua nyingine, aliwataka wajumbe wa Ukawa kurejea bungeni kwa ajili ya kujenga hoja wakiwa ndani badala ya kwenda nje na kusababisha hali ya wasiwasi nchini.

Alisema wakiwa ndani itakuwa rahisi kushauriana ili kufikia mwafaka wa Katiba mpya ya Watanzania.  
SOURCE: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa