Home » » WAKAZI MLIMWA C WAIGOMEA CDA

WAKAZI MLIMWA C WAIGOMEA CDA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WAKAZI wa Mlimwa C mjini Dodoma, wamepinga uamuzi wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) kuwaamuru wabomoe nyumba zao bila kuwalipa fidia.
Wakizungumza na Tanzania Daima Jumatano, walielezea masikitiko yao kwa kuitwa wavamizi kwenye eneo wanaloishi kihalali, huku wakisema hawana tatizo la kuhamishwa ila wanachohitaji ni CDA kuwalipa fidia kabla ya kuwahamisha.
Wamemlalamikia pia mwekezaji wa hoteli ya Africa Dream na kudai kuwa anawasababishia tabu kwa kuwahonga watendaji wa mamlaka na mwenyekiti wa mtaa huo.
Mkurugenzi Mtendaji wa CDA, Pascas Mulagili, akijibu tuhuma hizo, alisema wakati wanaanza zoezi la kuwatambua wavamizi walikubaliana mambo makuu matatu.
“Katika kuhalalisha ukaazi wao moja ilikuwa wakazi wote wa eneo hili ni wavamizi, pili tulikubaliana kuwapimia maeneo hayo na tatu tulikubaliana kuwa wananchi watakaojikuta wako wawili kwenye sehemu moja itabidi mmoja aondoke na hatalipwa fidia.
“Mambo yote matatu yaliyokuwa msingi wa kuamua kupima eneo husika yaliafikiwa, nawashangaa wanaoibuka kwa hoja ya kulipwa fidia jambo ambalo halikuwa makubaliano ya awali,” alisema mkurugenzi huyo.
Kwa mujibu wa Mulagili walichokifanya ni kutambua mipaka ya ile barabara na kuwawekea X na kuwapelekea taarifa ya kwamba wanatakiwa kuvunja nyumba zao na kupisha barabara.
Alisema baada ya wananchi hao kuona hali hiyo, waliamua kukimbilia mahakamani hatua ambayo mamlaka iliiona ni nzuri kwa kuwa wamekwenda kwenye chombo kinachosimamia sheria, kesi ambayo ilichukua zaidi ya miaka miwili.
Mulagili alisema muda waliowapa kimsingi umekwisha na hivi sasa wanajipanga kwenda kuwaondoa huku akisisitiza kwamba anatoa rai kwa wananchi wote wenye nyumba barabarani waondoke bila kusubiri matumizi ya nguvu ili kuwaondoa.
Alisema Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) inaendelea na zoezi la uchunguzi ili kuwabaini watu waliohusika na tuhuma za rushwa katika zoezi la ugawaji wa viwanja ambalo lilisimamiwa na uongozi wa serikali ya eneo husika na kuwachukulia hatua za kisheria.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa