Home » » HALMASHAURI SITA ZAKIUKA MASHARTI YA MFUKO WA JIMBO

HALMASHAURI SITA ZAKIUKA MASHARTI YA MFUKO WA JIMBO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Pamoja na Sheria ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo (CDTF), kuweka sharti la miradi itakayotekelezwa iibuliwe na wananchi, halmashauri sita nchini zimebainika kukiuka.
Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), iliyowasilishwa bungeni, inaonyesha kuwa Halmashauri hizo zilitumia Sh195.5 milioni kwa miradi ambayo haikuibuliwa na wananchi.
Aidha, halmashauri za wilaya tatu zilitumia Sh19.9 milioni za mfuko huo kugharimia posho za kujikimu nje ya kituo cha kazi, gharama za usafiri na posho za vikao kinyume cha sheria.
Kifungu cha 12 cha Sheria ya Mfuko wa Jimbo ya mwaka 2009, kinaeleza kuwa orodha ya miradi inayoweza kutekelezwa inatakiwa kuibuliwa na wananchi wanaoishi katika jimbo husika.
Pia Kifungu cha 10(4) cha sheria hiyo kinaitaka kila kata kuandaa miradi inayopewa kipaumbele na kuiwasilisha kwenye kamati ya mfuko wa jimbo kwa ajili ya kuidhinisha au kutoidhinisha miradi hiyo.
CAG Ludovick Utouh katika taarifa yake alisema tofauti na matakwa hayo ya sheria, miradi yenye thamani ya Sh195.5 milioni iliyotekelezwa mwaka 2012/2013 haikuwa na ushahidi kuwa iliibuliwa na wananchi. Halmashauri hizo na kiasi cha fedha kwenye mabano ni Iramba (Sh62.2 milioni), Chato (Sh21.6 milioni), Handeni (Sh32.7milioni), Sengerema (Sh12.8 milioni), Lushoto (Sh9 milioni) na Tabora Sh57 milioni.
CAG alisema Kifungu cha 19(2) cha Sheria ya Mfuko wa Jimbo kinaeleza kuwa, miradi itakayoibuliwa inaweza kuhusisha gharama za masomo, mipango na ubunifu au nyenzo za kiufundi kwa ajili ya miradi.
Halmashauri zilizotumia fedha za CDTF kulipana posho ni Ludewa iliyotumia Sh3.4 milioni kununua mafuta, Urambo iliyotumia Sh12.8 kwa ajili ya posho za safari na Kondoa iliyotumia Sh3.7 kulipana posho za vikao.
Katika kipindi hicho pia, halmashauri 66 hazikutumia kabisa kiasi cha Sh2.59 bilioni za mfuko wa jimbo, huku Halmashauri ya Bariadi ikiongozwa kwa kutotumia Sh248  milioni. Halmashauri nyingine ni Kilosa Sh190.7 milioni, Mvomero Sh116.3 milioni na Ilemela Sh106 milioni.
 Chanzo:MWANANCHI

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa