Home » » KAMATI KUU CCM YAKUNA KICHWA KUIKABILI UKAWA

KAMATI KUU CCM YAKUNA KICHWA KUIKABILI UKAWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimesema hakina haja wala mpango wa kuzungumza na wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), waliosusia Bunge la Katiba, badala yake watashughulika nao mitaani kwa kujibu mapigo yao.
“Hatuna mpango wa kuzungumza nao, lakini tuna mpango wa kushughulika nao mtaani… Tutaendelea kwenda huko wanakopita,” Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye aliwaambia waandishi wa habari mjini hapa jana na kuongeza:
“Nadhani waendelee kukaa barabarani... watu wenyewe hawajai mkononi, hiyo theluthi mbili inapatikana bila wao, kwa nini tuwabembeleze?”
Nnauye alikuwa akizungumzia mambo yaliyojadiliwa katika Kamati Kuu (CC) ya CCM ambayo ilikutana kwa dharura chini ya Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete na kupokea taarifa ya yaliyojiri ndani na nje ya Bunge Maalumu la Katiba.
Maelezo ya Nnauye yanaonyesha kuwa mjadala kuhusu Ukawa ulitawala mazungumzo ya kikao hicho hasa ikizingatiwa kwamba hakueleza jambo jingine lolote lililojadiliwa zaidi ya hilo.
Alisema CC imeipongeza sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM (Nec), chini ya Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana, kwa kujibu alichoita uongo na uchochezi unaoenezwa na Ukawa mitaani juu ya mchakato wa Katiba Mpya.
Sekretarieti hiyo imeshafanya mikutano mbalimbali ya hadhara Pemba na Unguja.
“CC imeitaka sekretarieti na wanachama wanaoitakia nchi yetu mema kuendelea kujibu kila uongo unaozungumzwa au kuenezwa… Ujibiwe kwa uzito unaostahili,” alisema.
Alisema pamoja na upungufu uliojitokeza, Kamati Kuu imeridhishwa na mwenendo na mchakato wa mabadiliko ya Katiba na kuwapongeza wajumbe waliobaki bungeni akisema wameonyesha uzalendo na kutanguliza masilahi ya nchi na waliosusia Bunge hilo wameonyesha kuwa hawana nia wala dhamira ya dhati ya kuhakikisha Watanzania wanapata Katiba bora kwa wakati.
Ukawa unaundwa na wajumbe kutoka vyama vya NCCR-Mageuzi, Chadema, CUF na baadhi ya wajumbe kutoka kundi la 201 ambao waliteuliwa na Rais Kikwete.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa