Home » » 'NANI ALIIDHINISHA MATUMIZI BUNGE LA KATIBA'

'NANI ALIIDHINISHA MATUMIZI BUNGE LA KATIBA'

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe ameitaka Serikali kueleza jinsi ilivyopata fedha za kuendesha Bunge Maalumu la Katiba kwa kuwa Bunge la Muungano halikuwahi kuziidhinisha.
“Hadi sasa Bunge (la Muungano), halijui bajeti yote ya Bunge Maalumu la Katiba. Halijui fedha kiasi gani zimetumika kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya miundombinu ya Bunge la Katiba,” alisema katika hotuba yake ya maneno 10, 910.
Fedha alizokuwa akihoji Mbowe ni zilizotumika kulipa posho, mishahara na stahiki mbalimbali za wajumbe na watumishi wa Bunge Maalumu hadi lilipoahirishwa Aprili 25, mwaka huu na hata litakaporejea Agosti 5, mwaka huu.
Wasiwasi wa Mbowe unalenga kupata majibu ili kuliepusha Taifa na balaa la ufisadi na wizi wa fedha za umma kama ilivyotokea mwaka 2005.
Mbowe alisema mwaka huo mabilioni ya fedha za umma yaliibwa kutoka katika Akaunti ya Malipo ya Nje (EPA), ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kwa ajili ya kugharimia kampeni za Uchaguzi Mkuu wa CCM na mgombea wake wa urais.
Alisema Serikali haijawahi kutoa makadirio ya matumizi kwa ajili ya shughuli za Bunge la Katiba licha ya kutakiwa kufanya hivyo mwaka jana na Kamati ya Bunge ya Katiba na Sheria wakati wa mjadala wa makadirio na matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria mwaka 2013/14.
Alisema fedha za Bunge la Katiba zilitakiwa kuidhinishwa kisheria kama inavyosema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kwamba fedha hizo zitatoka katika Mfuko Mkuu wa Hazina ya Serikali.
Alisema zilitakiwa kuidhinishwa na ama na Sheria ya Matumizi ya Serikali iliyotungwa mahsusi na Bunge au sheria iliyotungwa kwa mujibu wa Ibara ya 140 ya Katiba inayohusu mfuko wa matumizi ya dharura unaoanzishwa kwa ajili ya mambo ya haraka na dharura.
“Hata kama fedha za matumizi ya Bunge la Katiba zingeainishwa kama inavyotakiwa na Katiba, bado matumizi hayo yalitakiwa kuidhinishwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG),” alisema Mbowe.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa