Home » » Nundu: Vigogo serikalini walipewa nyumba na wageni

Nundu: Vigogo serikalini walipewa nyumba na wageni

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Waziri wa zamani wa Uchukuzi, Omar Nundu

Waziri wa zamani wa Uchukuzi, Omar Nundu jana aliikalia kooni Serikali kwa kuwakumbatia wageni na kuibua madai kuwa baadhi ya vigogo wa Serikali walipewa nyumba wakati wa kubinafsisha viwanda nchini.
Nundu ambaye ni Mbunge wa Tanga Mjini (CCM), alitoa kauli hiyo jana jioni alipokuwa akichangia bajeti ya Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda kwa mwaka 2014/15. “Hizi tax holiday (kipindi maalumu cha kusamehewa kodi) ziondolewe maana siyo tunasema maneno tu, umefika wakati sasa maneno yakae kando vitendo vifanye kazi, watu wamechukua viwanda kwa ajili ya kuvidhoofisha tu,” alisema.
“Tanga kule vimejaa chungu nzima (viwanda) na tunapoongelea mbolea, tena tunakuwa kama tunaongelea maji tu… Tunayajua mliyoyafanya. Vipo mlivyopewa kutoa viwanda vile. Ondoeni mawazo hayo msitupeleke mpaka tukasema mambo haya humu ndani,” alisema Nundu na kuongeza:
“Mnapewa vijijumba, watu wazima ovyoo, unapewa kijijumba halafu unadhalilisha nchi hapa! Mmeyafanya! Twende viwanda virudi tufanye kazi,” alisema Nundu bila kuwataja kwa majina waliopewa nyumba.
Nundu alisema uchumi duniani kote unategemea viwanda na kwamba pamoja na wizara kueleza mambo mengi ukweli ni kwamba hayatoshi na kuna mengi ya kufanya.
Utajiri wa magadi
Awali, akiwasilisha bajeti yake, Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda alisema uzalishaji wa magadi soda utaanza kuliingizia taifa Dola 320 milioni za Marekani (Sh520 bilioni) kwa mwaka kuanzia mwaka 2016/17.
Alisema mradi huo unaoendeshwa na Shirika la Maendeleo ya Taifa (NDC), unatarajia kuzalisha tani milioni moja za madini hayo na bidhaa nyingine za chumvi kwa mwaka. Alisema tafiti kuhusu wingi na ubora wa rasilimali ya magadi soda zilikamilika mwaka 2013/14 na kiasi cha tani bilioni 4.68 za magadi ambazo huongezeka kwa mita za ujazo milioni 1.86 ziligunduliwa.
Dk Kigoda alisema kiasi hicho kiligunduliwa katika Bonde la Engaruka na jitihada za kumtafuta mtaalamu mshauri zimeanza.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa