Home » » PIKIPIKI KUSAJIRIWA UPYA SASAKUPEWA NAMBA "T"

PIKIPIKI KUSAJIRIWA UPYA SASAKUPEWA NAMBA "T"

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Serikali imetangaza utaratibu mpya kwa usajili wa namba za pikipiki kutoka ‘T’ na sasa zitasomeka ‘TZ’ lengo likiwa ni kudhibiti vitendo vya uhalifu.
Hatua hiyo ilitangazwa bungeni mjini Dodoma jana na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya wakati akiwasilisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2014/15.
Uagizaji magari waongezwa makali
Waziri Mkuya alisema, Serikali inatarajia kuongeza kodi kwa magari yatakayoingizwa nchini yakiwa yametumika kwa zaidi ya miaka minane baada ya kubadilisha ukomo wa umri wa magari yasiyo ya uzalishaji (non-utility vehicles) na magari ya uzalishaji na yasiyobeba abiria (non-passanger utility vehicles), kutoka miaka 10 hadi minane.
Alisema hatua hiyo ina lengo la kulinda mazingira na kupunguza wimbi la uigizaji wa magari chakavu ambayo yanasababisha ajali, vifo na kuongeza gharama kwa kutumia fedha za kigeni kuagiza vipuri mara kwa mara.
Pendekezo hilo pia liliwasilishwa katika Bajeti inayomalizika lakini liliondolewa baada ya kuibua mvutano mkubwa bungeni na kusababisha Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kuingilia kati.
Waziri wa Fedha wakati huo, marehemu William Mgimwa alisema Serikali iliwasilisha pendekezo hilo ili kupunguza muda wa magari yaliyotumika kuingia nchini kwa lengo la kudhibiti magari chakavu, kutunza mazingira na kuwapunguzia wananchi mzigo wa kununua mafuta kwa kuwa yanatumia nishati hiyo kwa wingi.
Alisema Serikali inatekeleza hoja hiyo kwa kuwa hata Kenya na Uganda wameanza kufanya hivyo na kwamba ni mpango wa nchi nyingi.
Baada ya kuwasilisha muswada huo, Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Fedha na Uchumi, iliwasilisha maoni yake na kupinga pendekezo hilo la Serikali kwa kueleza kwamba uwezo wa wananchi wengi kununua magari mapya ni mdogo.
Akiwasilisha maoni ya Kamati, aliyekuwa mwenyekiti wake, Andrew Chenge alisema Serikali haikuwa na nia ya kuyaondoa barabarani magari yenye umri zaidi ya miaka 10, hivyo pendekezo hilo halikuwa na manufaa kwa taifa.
“Kamati inaamini kwamba sababu zilizofanya Serikali kuleta mapendekezo bungeni mwaka 2006 ya kutoza ushuru wa bidhaa za magari yenye umri zaidi ya miaka 10 bado zina nguvu hadi leo… Kamati inashauri umri wa magari yanayostahili msamaha uwe miaka 10 na siyo minane inayopendekezwa,” alisema.
Msimamo huo wa Kamati uliungwa mkono na Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, ambayo ilisema hoja ya Serikali katika eneo hilo ni dhaifu kwa kuwa wananchi wengi hata wabunge hawana uwezo wa kununua magari mapya na wala umri wa gari si kigezo pekee cha ubora.
Mvutano huo ulimlazimu Waziri Mkuu Pinda kuingilia kati na kueleza kwamba Serikali imekubaliana na maoni ya wabunge na kukubali umri wa magari yanayoingia nchini kubaki kuwa miaka 10.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa