Home » » SERIKALI YAPOKEA GAWIO LA BIL 1/KUTOKA TIPER

SERIKALI YAPOKEA GAWIO LA BIL 1/KUTOKA TIPER

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
SERIKALI imepokea gawio la sh bilioni 1. 275 kutoka Kampuni ya Mafuta ya Tanzania Petroleum Reserves Limited (Tiper), baada ya kampuni hiyo kupata faida baada ya kodi ya sh bilioni 6.06 kwa mwaka wa fedha 2013.
 Akizungumza muda mfupi baada ya kupokea hundi kwa niaba ya Serikali katika Ofisi ya Hazina jijini Dodoma mwishoni mwa wiki, Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dk Servarcius Likwelile, alisema fedha hizo zitasaidia kujazia kwenye mapungufu yaliyojitokeza katika bajeti ya mwaka 2013/2014.
 "Gawio hili kutoka Tiper litaisaidia Serikali kuziba mapengo yaliyobaki katika bajeti kutokana na ukweli kwamba hatukuweza kufikia malengo yetu katika ukusanyaji wa mapato. Tutazielekeza fedha hizi katika sekta zinazozihitaji zaidi. Usambazaji wake utategemea na mgawanyo wa bajeti ya mwaka 2013/2014 jinsi ilivyo,” alisema.
 Aliupongeza uongozi wa kampuni ya Tiper kwa utendaji bora ambao umeifanya kampuni huyo kuendelea kupata faida nzuri, kutengeneza ajira, kuhakikisha nchi ina kiasi cha kutosha cha akiba ya mafuta ya petroli na kuhakikisha kwamba wanahisa wote wawili wanapata magawio yao jinsi inavyotakiwa.
 Akizungumuza wakati wa hafla ya kukabidhi hundi hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Tiper, Daniel Belair, alisema mchango wa kampuni yake utasaidia katika kuchochea jitihada mbalimbali za maendeleo ya kijamii na kiuchumi nchini.
 "Mwaka 2013 ulikuwa ni mwaka bora kwa kampuni ya Tiper hususani katika utendaji wake ambapo kampuni iliweza kupata faida ya sh bilioni 8.8 kabla ya kodi na kuweza kulipa kodi ya mapato ya sh bilioni 2.74 kwa serikali.
 "Tiper imejidhatiti katika kuwekeza nyenzo za kisasa za kuhifadhia mafuta na itahakikisha kwamba mafuta ya petroli yanapatikana kwa urahisi kwa watumiaji wote wadogo na kubwa," alisema Beilar.
Alisema kampuni hiyo imewekeza zaidi ya dola milioni 10 za Marekani kwa ajili ya kuongeza uwezo wake wa sasa wa kuhifadhi mafuta ya mita za ujazo 141,000 hadi kufikia mita za ujazo 290,000 ifikapo mwaka 2015.
 Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Tiper, Profesa Abdulkarim Mruma, alisema kampuni hiyo inayomilikiwa kwa pamoja na Serikali ya Tanzania na kampuni ya Oryx Oil & Gas (OOG), kila mmoja akiwa na hisa za asilimia 50  imekuwa ikilipa gawio kwa serikali tangu 2009 kutokana na uwekezaji mkubwa wa sh bilioni 8.3.
 chanzo :Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa