Home » » BETTY MKWASA AMVAA MBUNGE BAHI

BETTY MKWASA AMVAA MBUNGE BAHI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MKUU wa Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma, Betty Mkwasa, amemlalamikia Mbunge wa Bahi, Omar Badwel (CCM), kwa kuwahamasisha wananchi kuharibu mazingira ikiwa ni pamoja na kufyeka msitu wa hifadhi ya taifa wa Chenene.
Akizungumza na vyombo vya habari juu ya uharibifu wa mazingira katika msitu huo, Mkwasa, alisema kuwa wapo wakulima ambao ni wahamiaji wanaokingiwa kifua na mbunge huyo kwa misingi ya kuangalia jinsi ya kulinda kura katika uchaguzi mkuu mwakani, bila kuangalia athari za mazingira.
Mkwasa, aliyasema hayo baada ya kuulizwa swali ni kwanini wananchi wa wilaya hiyo hususani wakulima, wamevamia msitu huo na kuanza kufyeka miti wakati msitu huo ni hifadhi.
Alikiri kuwepo kwa wananchi ambao ni wakulima waliovamia msitu huo na kuanza kufyeka miti kwa malengo ya kuendeleza kilimo, japo walishapewa tahadhari na kutakiwa kuondoka katika msitu huo.
“Wapo wakulima ambao walivamia hifadhi hiyo kwa lengo la kulima, lakini serikali imekuwa ikizuia, baada ya kuona hilo, watu wa hifadhi walilazimika kwenda kuweka mipaka kwa lengo la kuwataka wakulima hao kuondoka katika hifadhi hiyo…
“Kutokana na hali hiyo, wakulima walikuja ofisini kwangu kwa lengo la kuomba wasiondoke hadi hapo watakapokuwa wamevuna mazao yao, kutokana na hali ya ubinadamu, niliwashauri wavune kwanza mazao yao na baadaye wakimaliza kuvuna wasirudie tena kulima na badala yake waondoke katika msitu huo…
“Cha kushangaza, mbunge wa jimbo alikwenda katika msitu huo na kuwaambia kuwa wasiondoke na waendelee kulima, jambo ambalo limesababisha kuendeleza uharibifu wa mazingira kwa kiasi kikubwa, kwani kwa sasa wameanza kufyeka miti na kudai kuwa hawawezi kuhama kutokana na kauli ya mbunge wao,” alisema Mkwasa.
Hata hivyo, alisema kuwa kwa misingi ya sheria ya utunzaji wa mazingira, yeye na timu yake watahakikisha wakulima hao wanaondoka katika msitu huo mara watakapomaliza kuvuna mazao yao.
Kwa upande wake, mbunge Badwel alipoulizwa kuhusu hilo, alisema ni kweli wakulima hao ni wa siku nyingi wakiendeleza shughuli zao za kilimo na wakati wote serikali ilikuwa imelala.
“Haiwezekani watu ambao walianza kulima zaidi ya miaka 50 ukawaambia waondoke, kwani siku zote walikuwa wapi? Huwezi kuwaondoa watu kama kuku au bata, mimi nimewaambia hakuna sababu ya wao kuondoka hadi hapo serikali itakapokaa na wananchi na kutatua mgogoro huo,” alisema
 Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa