Home » » DK.NCHIMBI AISHUKIA DUWASA

DK.NCHIMBI AISHUKIA DUWASA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399
 
MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi, ametoa wiki moja kwa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira mjini Dodoma (Duwasa), kung’oa mara moja mifumo ya maji isiyotakiwa katika visima vilivyopo ndani ya viwanja vya maonyesho ya wakulima ya Nane Nane eneo la Nzuguni ili kuondoa mzozo uliopo.
Dk. Nchimbi, alitoa agizo hilo mjini hapa juzi, wakati wa mkutano wa maandalizi ya sherehe hizo za wakulima (Nanenane), Kanda ya Kati zinazotarajiwa kuzinduliwa Agosti Mosi, ulioshirikisha wadau mbalimbali.
Alisema ni suala la upuuzi na aibu kwa Duwasa na Umoja wa Wakulima Kanda ya Kati (Taso), ambazo zote ni taasisi za serikali, kuleta mzozo unaozorotesha utendaji kazi katika eneo hilo na maonyesho ya Nanenane ambayo hufanyika kila mwaka.
“Nimeshagazwa sana kuona kunatokea jambo kama hili, hapa kuna vitu ambavyo vinapingana, maana nichojiuliza ni kwanini Duwasa waingilie na kuingiza mifumo yao na kuondoa kasi ya huduma wakati ilipaswa kuhakikisha huduma ya maji inaboreshwa Nanenane?” alihoji Dk. Nchimbi.
Alifafanua kuwa mamlaka hiyo imeweka mfumo wake wa maji katika visima pamoja na matenki ya Taso na watu waliopo katika eneo hilo, lakini cha kushangaza maji hakuna na hivyo kukwamisha maonyesho.
Alisema itaonekana haina maana kama watakuwa wanawahamasisha wananchi kuchimba visima halafu wanakwamishwa na Duwasa, kutokana na wao kuweka mfumo ambao hauna maji na kwamba, masuala hayo ni ya kipuuzi na hawawezi kuendelea na malumbano wakati kuna mambo yanaharibika, ndio maana yeye kama rais wa mkoa, ameamua kutoa agizo mara moja na kuwapa wiki moja tu kulitekeleza.
Alisema haipendezi kwa mamlaka hiyo kuingia kimaslahi katika eneo hilo na kudhoofisha maonyesho hayo, badala yake waingie kwa kuboresha kwa pamoja na kuhakikisha ufanisi unapatikana.
Akitolea ufafanuzi suala hilo, Katibu Tawala Mkoa ambaye ni Mjumbe wa Bodi ya Duwasa, Rehema Madenge, alisema kuwa mamlaka hiyo inafanya kazi kwa mujibu wa sheria ya mamlaka za maji mijini, hivyo eneo la maonyesho Nzuguni wanahusika.
Sambamba na hilo, aliwataka wananchi wa Mkoa wa Dodoma na maeneo jirani, kushiriki kikamilifu katika maonyesho hayo licha ya kuwa kitaifa yanafanyikia Mkoa wa Lindi na kuondokana na dhana ya kutoyathamini kwa kuwa yanafanyika kikanda
Chanzo:Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa