Home » » MADIWANI CHADEMA WAFUNZA WAFUNZA WENZAO

MADIWANI CHADEMA WAFUNZA WAFUNZA WENZAO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MADIWANI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Mkoa wa Dodoma, wamewataka viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuachana na siasa za maji taka na wajikite kutatua umasikini wa Watanzania.
Kauli hiyo waliitoa juzi walipokuwa wakizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za gazeti hili baada ya kuwepo kwa taarifa kuwa wanapanga kujiengua CHADEMA muda wowote kuanzia sasa baada ya kununuliwa na CCM.
Diwani wa Kata ya Dodoma Makulu, Ally Bilingi, alisema uzushi huo unaoenezwa na viongozi wa CCM kwa kushirikiana na wafuasi wao, unadhihirisha ukomavu wa rushwa na ununuzi wa uongozi unaofanywa na chama hicho tawala.
“Umefika wakati wa makada wa CCM kuanza kuweweseka, mimi niliingia CHADEMA kwa mapenzi yangu mwenyewe baada ya kuona CCM hawana sera na wanaficha ukweli kutokana na kulindana katika ufisadi…
“Lakini najua wazi kuwa CCM ili uweze kushika madaraka ni lazima uwe mtu wa kutoa rushwa, viongozi wengi wapo katika madaraka kutokana na vitendo vya kununua nafasi hizo, watafute hoja za kuwaeleza Watanzania, lakini siyo siasa za maji taka za kuwashawishi watu, eti sisi madiwani wa Dodoma tunaweza kununuliwa,” alisema.
Diwani wa Kata ya Ipala, Hamisi Nghumba, alisema si mara ya kwanza viongozi wa CCM kumfuata na kutaka aondoke CHADEMA na kuhamia kwao.
“Wamekuwa wakinifuata na kuniahidi kunipa fedha nyingi, lakini nimewakatalia siku zote, CCM kwa sasa wanatafuta kila mbinu ya kusambaratisha CHADEMA Mkoa wa Dodoma, lakini kutokana na chama hiki kuota mizizi kwa sasa hawawezi,” alisema.
Diwani wa Viti Maalum, Jemima Salali, alisema kuwa kwa misingi ambayo ameishaiweke katika maeneo mbalimbali ndani ya chama, kamwe hawezi kuondoka CHADEMA.
Diwani wa Iyumbu, Ezron Kudugwa, alisema CCM kwa kutumia makada wao wanatafuta njia ya kudhoofisha viongozi wa ngazi za juu wa CHADEMA kwa kuwapandikizia uongo ili wakate tamaa.
“Kama viongozi wa juu katika chama wakisikia mambo kama hayo wanashituka, lakini kiukweli mimi pamoja na madiwani wenzangu kamwe hatuwezi kuondoka CHADEMA,” alisema
 Chanzo:Tanzani Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa