Home » » WANAOJIFUNGUA NYUMBANI WATOZWA 6,000/-

WANAOJIFUNGUA NYUMBANI WATOZWA 6,000/-

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
WAUGUZI wa Zahanati ya Izava, iliyopo Kata ya Segala, Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma, wamelalamikiwa kwa kitendo cha    kuwatoza sh 6,000 kwa kila mzazi anayejifungulia nyumbani.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Tanzania Daima Jumapili, wajawazito hao walisema kuwa wauguzi wa zahanati hiyo wamekuwa na tabia ya kuwatoza fedha hizo wanapojifungua nyumbani na kuwapeleka watoto hospitalini.
Mmoja wa wajawazito hao, Mwanaidi Bakari, alisema miongoni mwa sababu zinazowafanya wajifungulie nyumbani ni wauguzi  hao kuwataka waende zahanati wakiwa na wakunga wao wa jadi ili wawasaidie.
Alisema kutokana na hali hiyo, wajawazito waliamua kujifungua nyumbani  kwa kuona kwamba wauguzi wenye  taaluma wanashindwa kuwasaidia bila kuwategemea wakunga.
“Tunashangaa, kwa kitendo hicho wengi wetu tumeamua  kujifungulia nyumbani na wakunga wa jadi, lakini cha ajabu tunatozwa kiasi cha fedha sh. 6,000,” alisema Mwanaidi.
Mganga Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, James Charles, alisema si utaratibu wa serikali kutoza fedha hizo na kueleza kuwa ni kinyume na taratibu na kuwataka wananchi kutoa taarifa ili hatua za kisheria zifuatwe.
“Hatuwezi kuvumilia kitendo hicho, wanalipwa mishahara na serikali kwa ajili ya kuwahudumia wanajamii pindi wanapohitaji huduma za kiafya,” alisema Charles.
 Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa