Home » » BUNGE LA KATIBA LIENDELEE- MZIRAY

BUNGE LA KATIBA LIENDELEE- MZIRAY

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 

BARAZA la Vyama vya Siasa nchini, jana limetoa msimamo wake likitaka Bunge Maalumu la Katiba, liendelee na mchakato wa kutengeneza Katiba Mpya ambao upo kwa mujibu wa Katiba, sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Mwenyekiti wa baraza hilo, Bw. Peter Mziray, alisema shinikizo linalotaka Rais Jakaya Kikwete alivunje Bunge hilo haliwezekani kwani kufanya hivyo ni kukiuka sheria zilizopo.

Alisema wananchi wanapaswa kufahamu kuwa, suala la Katiba ni jambo nyeti na marais wengi duniani wanaogopa kuliweka suala hilo mezani ili lizungumzwe.

"Kikao kilichoitishwa na Kituo cha Demokrasia nchini (TCD), Agosti 2 mwaka huu, kilikutanisha viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa na hakikuwa rasmi hivyo waliosema tulikubaliana mchakato huu usimame watoe ushahidi wa maandishi au kupeleka suala hilo mahakamani," alisema.

Aliongeza kuwa, katika kikao hicho walikubaliana mambo mengi na jambo moja lililobaki lipo kisheria kwani unapoamua kufanya maridhiano lazima uweke silaha chini.

Wakati huo huo, Bw. Mziray alitoa taarifa za kuahirishwa kwa kongamano lililopangwa kufanyika mjini Dodoma Agosti 23-24 mwaka huu, ambalo lilikuwa na lengo la kujadili mchakato huo pamoja na changamoto zake.

Alisema kongamano hilo lililenga kuwashirikisha viongozi wastaafu wa awamu zilizopita, viongozi mbalimbali wa Serikali kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, viongozi wa dini, wazee wastaafu na wakuu wa usalama nchini.

"Tumeahirisha kongamano hili kutokana na kiongozi mmoja kuwa na udhuru; hivyo tumeona ni bora tuliahirishe kutokana na unyeti wa jambo hili kuwa na umuhimu mkubwa katika nchi yetu," alisema Bw. Mziray.

Bw. Mziray alisema uamuzi wa kuandaa kongamano hilo ulitokana na Kikao cha baraza hilo pamoja na vyama vya siasa kilichofanyika Agosti 2 mwaka huu na kutoa pole kwa familia ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi nchini (NEC), Jaji mstaafu Lewis Makame, aliyefariki juzi, jijini Dar es Salaam.

Chanzo;Majira

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa