Home » » MAMBO MATATU YATESA BUNGE LA KATIBA

MAMBO MATATU YATESA BUNGE LA KATIBA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mwenyekiti wa kamati namba nne, Christopher Ole Sendeka
 
Suala la Mahakama ya Kadhi limezidi kuleta mvutano mkali baada ya kamati ndogo iliyoundwa na Kamati ya Uongozi ya Bunge Maalum la Katiba, kujadili kipengele hicho pamoja na suala la uraia pacha na muundo wa Bunge, kushindwa kukamilisha taarifa yake. Kamati hiyo ambayo ilikuwa ikiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba, Samia Hassan Suluhu,  ilipewa jukumu la kuangalia masuala hayo baada ya kuzusha mvutano na mabishano makali na wajumbe kushindwa kufikia muafaka wakati wa mijadala kwenye kamati mbalimbali za Bunge hilo.
 
Akizungumza mjini Dodoma jana, Katibu wa Bunge Maalum, Yahya Khamis Hamad, alisema kikao cha Kamati ya Uongozi kilichoitishwa jana kilishindwa kujadili taarifa ya kamati hiyo ndogo baada ya kutokuwamo kwa taarifa inayohusu Mahakama ya Kadhi.
 
“Kamati ndogo ilipewa jukumu la kuangalia suala Mahakama ya Kadhi, uraia pacha na muundo wa Bunge, hata hivyo jana walipowasilisha walitoa taarifa pungufu na kusababisha wajumbe kuwarudisha wakamilishe,” alisema Hamad.
 
Alisema katika taarifa yao, kitu kilichoonekana kufanyiwa kazi kwa ukamilifu ni muundo wa Bunge pekee.
 
Hamad alieleza kwamba, kamati hiyo imepewa muda hadi Jumatatu ijayo iwe imekamilisha kazi hiyo na taarifa yao iwasilishwe Kamati ya Uongozi kwa ajili ya kufanyiwa kazi kabla ya kuanza vikao vya Bunge hilo Jumanne ya wiki ijayo.
 
Kamati 10 kati ya 12 za Bunge Maalum la Katiba kwa muda wa siku 15 zilikuwa zikijadili sura mbalimbali za Rasimu ya Katiba na kazi hiyo ilihitimishwa juzi.
 
Kwa sasa kazi inayofanyika ni wenyeviti wa kamati hizo kuwasilisha taarifa za mijadala hiyo kwa Kamati ya Uandishi, ambayo itaziandaa na kuziweka katika utaratibu wa maoni ya walio wengi na ya wachache, ambayo yatawasilishwa ndani ya Bunge zima Septemba 2, mwaka huu kwa ajili ya kusomwa na kuanza mjadala wa Bunge zima.
 
Wakizungumza na waandishi wa habari nje ya ukumbi wa Bunge jana, baadhi ya wenyeviti wa Kamati za Bunge Maalum, walisema wanatarajia kuwa masuala yaliyoleta mvutano mkubwa ndani ya mijadala ya kamati, yataendelea kutuletea mvutano mkali kwenye mjadala wa Bunge zima.
Mwenyekiti wa kamati namba nne, Christopher Ole Sendeka, alisema pamoja na mivutano huyo kamati yake ilimaliza kujadili rasimu na kukubaliana kupitisha kwa baadhi ya vifungu kwa kupiga kura.
 
“Kulikuwa na mjadala mkali katika masuala muhimu kama ardhi, haki za wakulima na wafugaji uraia pacha na muundo wa Bunge,” alisema Sendeka.
 
Hata hivyo, Sendeka alifafanua kwamba kwa siku kadhaa hakuwapo katika vikao vya kamati yake kutokana na kupata matatizo ya kifamilia.
 
“Pamoja na kuwa nje ya kamati, nashukuru wenzangu walijadili haya na kukubaliana kwa pamoja,” aliongeza.
 
Akizungumzia kuhusu kamati namba tatu, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Dk. Francis Kasabubu, alitetea misuguano iliyoibuka katika kamati  yake kwamba ni jambo zuri katika kupatikana kwa Katiba mpya.
 
“Kunapotokea misuguano na kupingana kwa wajumbe ni dalili nzuri, tofauti za kimtazamo inaleta afya hasa katika kazi ya kuandaa katiba mpya,” alisema.
 
Alisema kwa upande wa kamati yake, kuliibuka hali hiyo lakini walijaribu kuzungumza na mwishowe walipitisha mapendekezo yao yote.
 
Mwenyekiti wa kamati namba moja, Ummy Mwalimu, alisema kitu ambacho walipata nacho shida na kukosa ufumbuzi hadi jana ni suala la mfuko wa fedha wa pamoja.
 
“Tulikubaliana kwa pamoja kuweka pembeni suala hilo hadi tupate ufafanuzi wa kitaalamu kutoka Wizara za Fedha upande wa Tanzania Bara na upande wa Zanzibar, jambo la kufurahisha tulijadiliana vizuri na  ibara zote tumezipitia na kufanya maboresho pale inapotakiwa,” alisema Mwalimu.
 
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa