Home » » MGAWANYO WA MAPATO WATIKISA BUNGE MAALUMU

MGAWANYO WA MAPATO WATIKISA BUNGE MAALUMU

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Samwel Sitta akifafanua jambo  

Hoja kuhusu mgawanyo wa mapato ya muungano imeendelea kulitikisa Bunge Maalumu la Katiba na jana watendaji wakuu wa wizara za fedha wa muungano na Zanzibar pamoja na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Profesa Benno Ndulu walitua Dodoma kuweka mambo sawa.
Vigogo hao wa fedha jana walikutana na baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu, kujaribu kupata mwafaka wa jinsi suala hilo litakavyowekwa kwenye Katiba Mpya.
Bunge la Katiba limelazimika kuwaita Dodoma watendaji hao ili kusaidia kukwamua mgogoro wa mapato ya muungano, ambao uliwagawa wajumbe wa kamati za Bunge hilo wakati wa mjadala wa sura ya 14 kwenye Rasimu ya Katiba.
Pamoja na Profesa Ndulu, wengine waliokuwapo ni Katibu Mkuu Hazina, Dk Servacius Likwelile na mwenzake kutoka Zanzibar, Mussa Omar ambao walikuwa na kibarua kigumu cha kupunguza ufa uliowatenga wajumbe wa Bunge hilo katika misingi ya Ubara na Uzanzibari.
Sura ya 14 ya rasimu ndiyo inayozungumzia masuala ya mapato ya muungano na mgawanyo wake.
Suala la mgawanyo wa mapato ni moja ya mambo manne magumu yaliyosababisha mvutano mkubwa katika kamati za Bunge hilo kiasi cha kusababisha Kamati ya Uongozi ya Bunge Maalumu kuunda kamati ndogo ili kulifanyia kazi.
Kutokana na kusababisha mivutano hiyo, Kamati Namba Moja iliamua kutolijadili kabisa suala hilo na badala yake, kuomba uongozi wa Bunge uwalete watendaji wakuu wa masuala ya fedha ili watoe mwongozo wa kuwawezesha wajumbe kujadili na kupata mwafaka wa jinsi fedha zitakavyoweza kusimamiwa na kugawanywa. Mwenyekiti wa kamati hiyo ambaye pia ni Naibu Waziri - Ofisi ya Makamu wa Rais, Ummy Mwalimu alisema walishindwa kupigia kura sura ya 14 baada ya kuona ina utata.
“Ni kweli hatukupigia kura sura ya 14 pekee, tuliona ina utata mkubwa ambao unahitaji ufafanuzi wa kina na bila shaka baada ya semina ya leo (jana) tutakutana kufanya uamuzi,” alisema Mwalimu.
Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Hamis Hamad alisema: “Kamati zote zimemaliza kazi, isipokuwa Namba Moja haikupigia kura sura ya 14 wakitaka ufafanuzi wa kitaalamu, ndiyo maana tumewaleta wataalamu leo.”
Alisema pamoja na kupigia kura sura hiyo, lakini hata kamati nyingine zilionekana kutoelewa vizuri sura hiyo, hivyo ujio wa wataalamu ulilenga kuwawezesha kujadili sehemu hiyo ya Katiba wakiwa na uelewa mpana.
Habari zinasema sura iliyojitokeza kwenye mijadala ya kamati zote 12 ilihamia kwenye semina hiyo, ambako ufa ulidhihirika baina ya wajumbe wa pande hizo mbili za muungano, lakini watendaji hao kwa kushirikiana na wataalamu wengine walifanikiwa kutoa mwelekeo wenye matumaini.
Hoja zilizojiri
Habari kutoka ndani ya kikao hicho zinasema hoja kubwa zilizojitokeza zilihusu uwiano wa mgawanyo wa mapato, kuanzishwa kwa tume ya pamoja ya kusimamia mapato na Zanzibar kuruhusiwa kukopa fedha nje na katika mashirika ya kimataifa bila kupata ridhaa ya Hazina.
Hivi sasa Zanzibar inapata asilimia 4.5 ya mapato ya muungano huku Tanzania Bara ikipata asilimia 95.5 kutokana na wingi wa idadi ya watu na eneo lake kijiografia, suala ambalo limekuwa likilalamikiwa kwa muda mrefu na Wazanzibari kwamba wananyonywa.
Hata hivyo, mmoja wa wajumbe alinukuliwa akizungumza katika kikao hicho kwamba kanuni ya mgawanyo wa mapato inayotumiwa sasa ilitokana na ushauri wa kitaalamu uliotolewa na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) na kwamba unaweza kupitiwa upya ikiwa kutakuwa na haja hiyo. Mmoja wa wajumbe kutoka Zanzibar alinukuliwa akihoji kwa nini upande huo wa muungano ambao ni nchi kamili usipewe asilimia 50 ya mapato yatakayopatikana katika mfuko huo.
“Katibu Mkuu (Likwelile) aliposimama kujibu hakukataa lakini alisema kiwango cha asilimia pia kinazingatia uwekezaji kwenye mfuko husika na kwamba kama uwekezaji ni sawa, basi hakuna shaka kwamba hiyo asilimia 50 inawezekana,” kilisema chanzo chetu.
Kuhusu suala la mfuko wa pamoja, habari zinasema wajumbe wengi walionekana kuwa na mwelekeo wa pamoja lakini walikosoa kutoanzishwa kwake hadi sasa, licha ya kwamba suala hilo liliamuliwa miaka 14 iliyopita.
Katika Kamati Namba Mbili, suala la tume ya pamoja limeongezwa na kupewa Ibara ya 221B, huku ikipendekezwa kwamba tume ya pamoja ya fedha iwe na wajumbe wasiozidi saba watakaoteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kushirikiana na Rais wa Zanzibar. Watatu watatoka Zanzibar na wanne Tanzania Bara.
Tume hiyo, pamoja na mambo mengine inapendekezwa iwe na jukumu la kuchambua mapato na matumizi yanayotokana au yanayohusu utekelezaji wa mambo ya Muungano na kutoa mapendekezo kwa serikali zote mbili kuhusu mchango na mgawo wa kila mojawapo wa serikali hizo.
Hata hivyo, ndani ya kamati kadhaa, wajumbe kutoka Tanzania Bara walikuwa na msimamo kwamba lazima Zanzibar ipate idhini ya Hazina kabla ya kukopa fedha nje kwani Serikali ya Muungano ndiyo mdhamini mkuu wa mikopo hiyo.
“Hatuwezi kuruhusu Zanzibar wakope wanavyotaka, lazima Serikali ya Muungano ijiridhishe kwamba masharti yote kuhusu ukopaji yamezingatiwa, vinginevyo tunaweza kuiingiza nchi katika matatizo makubwa,” kilisema chanzo kingine.
Akizungumzia kikao hicho, Mwalimu alisema semina waliyoipata itawawezesha kufanya uamuzi sahihi watakapokuwa wakijadili sura hiyo ya 14.
Mbunge wa Mbarali, Modestus Kilufi alisema kuwa semina hiyo imemsaidia kwa kiasi kikubwa ingawa ilikuja kwa kuchelewa.
Kwa upande wake Mbunge wa Dimani, Abdallah Sharia Ameir alisema semina ya jana ingawa imechelewa itatoa mabadiliko makubwa
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa