Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), jana ulikuwa gumzo katika
kikao cha Kamati Kuu (CC) ya Chama cha Mapinduzi (CCM) mjini hapa.
Mjadala katika kikao hicho ulijikita kusaka
mwafaka na moja ya maazimio yake, ni kuendelea majadiliano ya kusaka
maridhiano baina ya chama hicho na vyama vinavyounda Ukawa ili kukwamua
mchakato wa Katiba Mpya.
Kamati hiyo ilitoa maelekezo hayo baada ya kupokea
na kujadili taarifa kuhusu mchakato wa Katiba Mpya pamoja na taarifa za
mazungumzo ya kusaka maridhiano yaliyofanyika katika ngazi tofauti na
kwa nyakati tofauti.
Habari kutoka ndani ya CC iliyofanyika chini ya
uenyekiti wa Rais Jakaya Kikwete ziliyataja mazungumzo hayo kuwa ni yale
yaliyowahusisha makatibu wakuu wa vyama, yale yaliyofanyika chini ya
uratibu wa Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) na yaliyoratibiwa na
Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi.
“Kamati Kuu imemwagiza Katibu Mkuu (Abdulrahman
Kinana) kuendelea na jitihada za mazungumzo tena kwa uzito zaidi, maana
sisi (CCM) hatujawahi kukataa mazungumzo na tumeona baadhi ya
mapendekezo yao yana maana sana na yana nafasi yake katika mchakato
huu,” kilisema chanzo chetu kutoka ndani ya kikao hicho.
Chanzo chetu kilimnukuu Rais Kikwete akisema kwa
kuzingatia mchakato wa Katiba ulivyo, si vyema kupuuza kila kinachosemwa
na wapinzani kwani baadhi ya mawazo yao yanaweza kuongeza thamani
katika mchakato huo.
Habari zinasema maelekezo ya kuwashawishi Ukawa
ili warejee katika meza ya mazungumzo na baadaye bungeni, ni matokeo ya
mjadala ulioonyesha kutokuwapo kwa uwezekano wa kupatikana kwa theluthi
mbili ya kura kutoka Tanzania Zanzibar wakati wa kupitisha Rasimu ya
Katiba katika Bunge Maalumu.
“Baada ya hesabu kupigwa ilionekana kwamba
tunahitaji kura 141 kutoka Zanzibar na kwa hesabu za pale kikaoni
ilisemekana kwamba tayari tuna kura za uhakika 135, kwa hiyo
zinazotafutwa ni kura sita tu,” kilisema chanzo kingine na kuongeza:
“Kutokana na hilo ilikuja hoja kwamba hata kama
tungepata hizo kura sita mchakato kwa ujumla wake utakosa uhalali wa
kisiasa kwa sababu Ukawa hawamo kwenye kikao na hakuna dalili ya
kurudi.”
Kwa mujibu wa habari hizo kulikuwa na mwelekeo
unaomsukuma Rais Kikwete kukutana na kundi hilo linaloundwa na vyama vya
siasa vya Chadema, NCCR Mageuzi na CUF ili kuona kama wajumbe wake
watarejea bungeni.
Hata hivyo, kikao hicho kiliambiwa kwamba Ukawa
hawajawahi kuomba kukutana na Rais licha ya kwamba amekuwa tayari wakati
wote. Hivyo kikao kilimwagiza Katibu Mkuu Kinana aendelee na jitihada
za mazungumzo kwa kuyatilia maanani kuliko ilivyokuwa mwanzo.
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye
alipoulizwa kuhusu yaliyojiri kwenye kikao hicho hakuwa tayari
kuzungumza na badala yake alisema taarifa rasmi itatolewa leo saa 2:00
asubuhi atakapokutana na waandishi wa habari Makao Makuu ya CCM, Dodoma.
Kabla ya kuanza kwa kikao hicho, Rais Kikwete, Makamu wake
wawili; Philip Mangula na Dk Ali Mohamed Shein pamoja na Katibu Mkuu,
Kinana walikuwa na kikao kinachokadiriwa kuchukua zaidi ya saa moja.
Wakati kikiendelea, Katibu wa Siasa na Uhusiano wa
Kimataifa wa CCM ambaye pia ni Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Asha-Rose
Migiro aliitwa kushiriki kikao hicho kilichokuwa kikifanyika kwenye
ofisi zilizopo karibu na ukumbi wa mikutano.
Baada ya mazungumzo hayo, Rais Kikwete aliwaongoza
viongozi wake kuingia ukumbini saa 9:34 alasiri na baada ya kuketi na
kupewa taarifa akidi ya wajumbe, alihoji aliko Meya wa Ilala, Jerry
Silaa, mjumbe pekee ambaye hakuhudhuria.
Kinana alisema wajumbe wa kikao hicho walikuwa 33 na kwamba Silaa yuko Arusha kwa ruhusa maalumu.
Rais Kikwete kabla ya kuwaondoa waandishi wa
habari waliokuwa ukumbini alisema: “Ndugu zangu sina ajenda mfukoni,
bali ni kikao cha kawaida tu katika utaratibu wetu, kikao kimefunguliwa
rasmi, naomba waandishi wa habari mtupishe.”
Chanzo;Mwananchi
Chanzo;Mwananchi
0 comments:
Post a Comment