Home » » ACT-TZ: WABUNGE MKATAENI PINDA BUNGENI

ACT-TZ: WABUNGE MKATAENI PINDA BUNGENI

 CHAMA cha Alliance for Change and Transparency (ACT-Tanzania), kimewaomba wabunge wote kuunganisha nguvu zao katika Bunge lijalo ili kupiga kura ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu, Bw. Mizengo Pinda, kama Rais Jakaya

Kikwete atashindwa kutekeleza maazimio ya Bunge likiwemo la kumwajibisha na kutengua uteuzi wa Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Bw. Samson Mwigamba, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema upo umuhimu wa wabunge wote kuunganisha nguvuzao bila kujali itikadi za vyama ili kumshinikiza Rais Kikwete atekeleze maazimio waliyoyatoa kwa kupiga kura ya kumkataa Bw. Pinda ili iwe fundisho kwa viongozi wengine.

“Bunge ni sauti ya wananchi na ndio maana linatoa maelekezo, linatunga sheria na kuisimamia Serikali, hivyo ni chombo muhimu na ndio mhimili mkubwa zaidi kuliko mihimili yote likiwa na uwezo wa kumwondoa Rais sasa iweje maazimio yake yasitekelezwe,” alisema Bw. Mwigamba.

Alisema maazimio ya Bunge yametokana na ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kuwahoji viongozi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), lakini Rais ameshindwa kuchukua hatua badala yake jambo hilo linafanyiwa uchunguzi.

“Bunge likipiga kura ya kumwondoa Bw. Pinda, litajiwekea heshima kubwa ya kutambulika kama mhimili mkubwa zaidi kuliko mihimili mingine,” alisema.

Aliongeza kuwa, kama vyombo vinavyowachunguza viongozi ambao bado wanaendelea na kazi vitathibitisha kuwa hawana makosa, Rais Kikwete yupo tayari kuukubali uchunguzi huo na kuupuuza ule wa Kamati ya Bunge.

“Hakuna mtu asiyejua kuwa Mawaziri walioondolewa baada ya kusitishwa kwa Operesheni Tokomeza akiwemo Bw. Shamsi Vuai Nahodha, Dkt. Emmanuel Nchimbi, Balozi Hamisi Kagasheki ambao wote hawakushika silaha wala kuua; lakini Rais alitengua uteuzi wao mara moja kutokana na Wizara zao kuhusishwa na matukio hayo.

“Inashangaza kuona Rais anapata kigugumizi kuhusu suala la Escrow na kushindwa kutekeleza maazimio ya Bunge kama lilivyoshauri... Rais hana chombo kingine cha uchunguzi zaidi ya TAKUKURU na CAG,” alisema.

Alisema maazimio yote ya Bunge, yamelenga kulisaidia Taifa si vinginevyo sasa iweje Rais alichukua maamuzi ya haraka katika Operesheni Tokomeza, lakini anashindwa kuwawajibisha Mawaziri walioguswa na sakata la Escrow?

Chanzo:Majira

 Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa