Home » » MAHAKAMA YA KADHI UTATA

MAHAKAMA YA KADHI UTATA

Wajumbe wa kamati tatu za Kudumu za Bunge ambazo wenyeviti wake wanatakiwa kuvuliwa nyadhifa zao kutokana na kuhusika katika kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow, ‘wanasuasua’ kuwaondoa na kuchagua viongozi wengine.

Kwa nyakati tofauti wajumbe wa kamati hizo ambazo ni Bajeti, Nishati na Madini na Katiba, Sheria na Utawala wamekuwa wakishangazwa na hatua za wahusika hao kuendelea kujitambulisha kuwa ni wenyeviti, sambamba na kuongoza vikao vya kamati hizo, wakati wakijua wazi kuwa hawatakiwi kufanya hivyo.

Wenyeviti wanaotakiwa kuachia nyadhifa zao ni Victor Mwabalaswa (Nishati na Madini), William Ngeleja (Katiba) na Andrew Chenge (Bajeti).

Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashilillah aliliambia gazeti hili jana kwamba jukumu la kuwaondoa wenyeviti hao lipo mikononi mwa wajumbe wa kamati hizo, kwamba kama wakishindwa Spika wa Bunge atachukua jukumu hilo.

Katika mkutano wake wa 16 na 17, Bunge liliazimia kuwa watu walioshiriki katika kashfa ya miamala ya Akaunti ya Escrow wakiwepo viongozi wa Kamati hizo tatu, wachukuliwe hatua za haraka na Kamati husika za Bunge kabla ya kuanza kwa mkutano wa 18 wa Bunge unaotarajiwa kuanza Januari 27 mwaka huu.

Akinukuu azimio hilo Kashilillah alisema, “Wajumbe husika ndiyo wanaotakiwa kuwaondoa wenyeviti hao, hilo ni lazima mlitambue jamani. Waulizeni ni lini watafanya hivyo.”
Alisema ndiyo maana kamati ikiwa haina mwenyekiti, wajumbe wenyewe huchagua mmoja kati yao kwa ajili ya kuongoza kikao cha kamati.

“Spika hawezi kumwondoa mwenyekiti wa kamati husika, anachoweza kufanya Spika ni kumhamisha mwenyekiti kutoka kamati moja kwenda nyingine. Akifanya hivyo maana yake ni kwamba mwenyekiti husika anapoteza sifa za kuwa mwenyekiti,” alisema.

Alisema jambo hilo Spika Makinda anaweza kulifanya kama wajumbe wa kamati hizo tatu zitashindwa kuchagua wenyeviti wengine mpaka kufikia siku ambayo utaanza mkutano wa 18 wa Bunge.

Kuhusu Chenge ambaye aliteuliwa na Spika Makinda kuwa mwenyekiti wa kamati ya Bajeti alisema, “Chenge aliteuliwa katika kipindi cha mpito ambacho kikiisha atachaguliwa mwenyekiti mwingine. Hivyo naye anaweza kuondolewa tu na wajumbe wa kamati.”

Mvutano katika kamati

Taarifa kutoka ndani ya kamati ya Bajeti zilieleza gazeti hili  kwamba, juzi kamati hiyo ilikutana na Wizara ya Maji na Uchukuzi na Chenge alijitambulisha kama mwenyekiti, jambo ambalo liliwashangaza wajumbe wa kamati hiyo.

“Tumeshangazwa jinsi alivyojitambulisha kwa sababu awali kamati tulikubaliana kuwa akae pembeni na kumwachia makamu mwenyekiti, Dk  Limbu (Festus) kuongoza vikao vya kamati. Inavyoonekana ni kama anang’ang’ania nafasi hii,” alisema mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo.

Mjumbe mwingine wa kamati hiyo alisema, “Ilitushangaza kwa sababu Dk Limbu alikuwapo na kamati ndiyo iliamua kuwa yeye awe mwenyekiti wetu kwa muda. Hili jambo linatuchanganya na ni vyema likapatiwa ufumbuzi.”

Alisema wajumbe wa kamati wanashindwa kuchukua hatua zaidi kwa sababu Chenge aliteuliwa kushika nafasi hiyo na Spika wa Bunge, Anne Makinda na kwamba yeye ndiyo mwenye mamlaka ya kumwondoa.

Mapema wiki hii, Dk Limbu alikaririwa na gazeti hili akisema, “Suala la Chenge linasubiri uamuzi utakaotolewa na  Spika wa Bunge, Anne Makinda.

“Kamati imeamua kwa busara Chenge akae pembeni na makamu mwenyekiti aongoze vikao huku ikisubiri hatua atakazozichukua Spika (Makinda),”

Kwa upande wake Ngeleja aliliambia gazeti hili kwamba anaendelea kushikilia nafasi hiyo kwa maelezo kuwa uchunguzi wa suala hilo bado unaendelea, ikithibitika ndipo Bunge litachukua uamuzi  ambao alidai yupo tayari kuutekeleza
Akizungumzia sakata hilo Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Gosbert Blandes alisema kuwa wamekwama  kutekeleza maagizo ya Bunge ya kumuondoa kwenye madaraka Ngeleja, baada ya kukosa mwongozo ndani ya kanuni.

“Kamati ilijadili kwa kina suala hilo kwamba ni vipi tunaweza kulishughulikia, tulipata utata mkubwa sana hatujaona kanuni ambayo tunaweza kuitumia, hivyo Ngeleja anaendelea kuongoza vikao kihalali,” alisema Blandes.

Alisema bado hawajapokea mwongozo wowote kutoka kwa spika, hivyo wanaendelea kusubiri huku wakijadiliana kwa amani tofauti na inavyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari.

“ Kamati inaendeshwa kwa mujibu wa sheria, hakuna mtafaruku wowote kwa pamoja tulijadiliana na kuridhia mwenyekiti aendelee na majukumu yake hadi hapo tunakapopata mwongozo,” alisema Blandes.

Kwa uapnde wake Mwabalaswa alisema, “Kamati haina jukumu hilo ambalo Katibu (Kashilillah) amekueleza, ila kama amekueleza hivyo sawa tu.”

Wabunge walia na Profesa Muhongo
Katika hatua nyingine wabunge walikosoa kitendo cha Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kuendelea na kazi licha ya maazimo ya Bunge kuitaka mamlaka ya uteuzi kumwajibisha.

Mbunge wa Ludewa (CCM), Deo Filikunjombe alisema, “Profesa Muhongo anaweza kuwa anafaa kufanya kazi nyingine lakini si hii na naomba ieleweke kwamba maazimio yale si ya Bunge bali ni ya wananchi hivyo lazima yakatekelezwa.”

Aliongeza: “Lakini atafanya kazi na nani (Muhongo)? Bajeti yake ataipitisha nani? Tutamwachia hatutampa ushirikiano.”

Filikunjombe ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya PAC alisema, “Profesa Muhongo anamwaibisha Rais (Jakaya Kikwete) na anampa wakati mgumu sana.”

Mbunge wa Viti maalumu (Chadema), Esther Matiko alisema, “Rais Kikwete alishasema kuwa fedha za IPTL siyo za Umma hivyo kwa kauli yake hii ni dhahiri hatachukua maamuzi ya utekelezaji wa maazimio ya Bunge.”

“Ila cha kushangaza na kuona jinsi hawa CCM  wanacheza na akili za Watanzania, Swali la msingi fedha si za Umma kwa nini wanatumia fedha za umma kushughulikia masuala binafsi,” alisema Matiko.
Aliongeza: “Rais Kikwete kwa kofia ya Mwenyekiti wa CCM wakiwa katika kikao cha Kamati Kuu yao huko Zanzibar wamebariki utekelezaji wa maazimio ya Bunge...upande mmoja Rais Kikwete anakana si fedha za umma upande mwingine anakubari maazimio ya Bunge hii inawachanganya Watanzania na wasijue msimamo wa Rais Kikwete ni upi.”

Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msingwa alisema, “Kutochukua uamuzi ni udhaifu wa taasisi ya Rais na ni ombwe la uongozi...ndiyo maana ana sita sita kuchukua uamuzi.”

Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi), Agripina Buyogela alisema, “Ukimya wa Rais unatupa mtihani ina maana hakuna mtu mwingine anayeweza kuwa Waziri wa Nishati na Madini mpaka ang’ang’aniwe Profesa Muhongo.”

Mbunge wa Mgogoni (CUF), Kombo Khamis Kombo alisema, “Ni jambo la dharau kwa wabunge na wananchi. Haiwezekani yatolewe maazimio lakini hayatekelezwi. Huyo Muhongo atachunguzwa vipi wakati bado anaendelea na wadhifa wake wa uwaziri.”
 Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa