WANAFUNZI 84 wa Chuo Kikuu UDOM wanashikiliwa na Polisi kwa tuhuma za kuhamasisha uvunjifu wa amani chuoni hapo.
Wanafunzi
hao walikamatwa wakifanya maandamano kutoka chuoni hapo kuelekea katika
ofisi mbalimbali za viongozi wa Serikali zilizopo Dodoma mjini majira
ya saa kumi na moja alfajiri jana.
Kamanda
wa Polisi mkoa wa Dodoma, David Misime alisema wahusika wa vurugu hizo
ni wanafunzi wa programu maalumu ya diploma ya ualimu.
Imeelezwa
kuwa awali wanafunzi hao juzi walifanya kikao ambapo walitoka na
maazimio ya kudai ongezeko la posho ya chakula na kupinga kucheleweshwa
malipo hayo.
Pamoja
na kutoka na madai hayo yaliyofikishwa kwa uongozi, uongozi uliwaeleza
kuwa wenye mamlaka ya kuzungumzia suala la kuongezewa posho ni Bodi ya
Mikopo na siyo chuo na kuwataka kufuata taratibu kuwasilisha madai yao.
Hata
hivyo, walielezwa kuwa hundi kwa ajili ya fedha za posho zao
zimeshasainiwa na kuwasilishwa benki ili waweze kuanza kupewa posho zao,
lakini hawakuridhika.
“Hata
hivyo, wanafunzi hao hawakuridhika na usiku wakaanza kuhamasishana
kufanya maandamano jambo ambalo ni kosa kisheria,” alisema Kamanda
Misime.
Aliongeza
kuwa, wanafunzi hao wamehojiwa kulingana na ushahidi ambao umekusanywa
na wamefikishwa mahakamani kwa kosa la kufanya maandamano yasiyo na
kibali.
Aidha,
alisema viongozi waliohamasisha uvunjifu huo wa sheria baadhi yao
wamekamatwa na baadhi wanaendelea kutafutwa ili nao waweze kuchukuliwa
hatua stahiki.
Ushahidi
uliokusanywa unaonesha jinsi viongozi hao wameshiriki kuhamasisha
kupitia vikao rasmi na visivyo rasmi, katika vikundi, kupita katika
mabweni na kutuma ujumbe mfupi wa simu (SMS).
Kamanda
huyo wa Polisi alitoa wito kwa wanafunzi hao kutumia taratibu
zilizowekwa na Serikali na Chuo kuwasilisha malalamiko yao ngazi kwa
ngazi na siyo kufanya vitendo vya kuvunja sheria ambavyo
vitawasababishia kupambana na vyombo vya dola.
Wanafunzi
hao ambao ni wa programu maalumu kwa ajili ya walimu wa masomo ya
Hesabu, Fizikia, Kemia, Baiolojia na Tehama yenye wanafunzi zaidi ya
3,000 wanasema wataendelea na maandamano na mgomo wakitaka kumuona Rais
au Waziri Mkuu ambao ndio wamekuwa wakihimiza programu hiyo maalumu.
Mmoja
wa wanafunzi hao, Yuda Mases akizungumza na gazeti hili alisema
maandamano yao yaliyokuwa ya amani yalikumbana na vikwazo vya polisi
ambavyo vilifanya waingie mjini kwa mtindo wa makundi.
Alisema
wenzao wapatao 100 akiwemo Rais na Waziri Mkuu wa Serikali ya Udom
programu maalumu wametiwa mbaroni katika juhudi za wazi za wanafunzi hao
kutaka serikali iwaangalie kutokana na kukosa fedha za chakula ambazo
zimechukuliwa na Chuo Kikuu cha UDOM.
“Tangu
Novemba 8, mwaka jana tumefika hapa tumelipwa Sh 367,500 kama hela ya
chakula kwa siku 60 kamili, lakini fedha hizo zilikatwa na UDOM Sh
282,500 kama Direct Cost na hii imeleta shida kwa wanafunzi,” alisema
Moses ambaye amedai kuwa kwa sasa kila siku mbili watu wanaanguka kwa
kukosa chakula.
Alisema
maandamano yao ni kutaka kuwaambia viongozi waliosimamia programu hiyo
maalumu Rais Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu Mizengo Pinda waone haki
inatendeka kuhusu fedha, malazi, vitabu na vitamkwa (vilivyoorodheshwa
katika barua za kuwaita).
Alisema
kwamba programu hiyo ina watu takribani 3,000 wakiwa wametawanyika
katika vitivo vitatu vya Tehama, Elimu na Sayansi Jamii.
Makamu
Mkuu wa chuo hicho, Profesa Idrisa Kikula hakupatikana kuzungumzia
suala hilo, kwani alipotafutwa ilielezwa yupo kwenye kikao.
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
0 comments:
Post a Comment