Na. Johary Kachwamba - MAELEZO, DODOMA
JAMII imetakiwa kutoa ushirikiano kwa jeshi la polisi nchini
katika kutoa taarifa zitakazo fanikisha kukamatwa kwa wote walioshiriki mauaji
ya watu wenye ulemavu wa ngozi nchini.
Wito huo umetolewa na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani Mhe.
Pereira Silima bungeni mjini Dodoma alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mhe.
Al -Shaimaa Kwegyir, Mbunge wa Viti Maalum aliyehoji kuchelewa kwa taarifa ya
kupatikana kwa mtoto mwenye ulemavu wa ngozi, Pendo Emmanuel.
“Pendo alitekwa kutoka mikononi mwa mama yake mzazi, hii
changamoto ni kubwa sana, tunaomba jamii itusaidie kutoa taarifa zitakazo
saidia kufanikisha kukamatwa kwa wahusika, tushirikiane kwa pamoja kukomesha
tatizo hili” alisema Mhe. Silima
“tangu kutekwa kwa mtoto Pendo watu 14 wanashikiliwa na jeshi la
polisi akiwemo baba mzazi, uchunguzi bado unaendelea na watuhumiwa watafikishwa
mahakamani hivi karibuni, ila Pendo bado hajapatikana” aliongezea Mhe. Silima
Aidha akijibu Swali la msingi la Mhe. Salumu Barwany, Mbunge wa
Lindi Mjini, aliyehoji idadi ya kesi za mauaji ya walemavu wa ngozi na sababu
za kuchelewa kutolewa hukumu. Mhe. Silima alisema kesi 10 zinaendelea
kisikilizwa mahakama mbalimbali
“kati ya mwaka 2006 hadi 2015 jumla ya matukio 56 ya uhalifu dhidi
ya watu wenye ulemavu wa ngozi yaliripotiwa nchini. Matukio 41 yalihusisha vifo
43, matukio 13 yalihusisha majeruhi 13 na matukio 2 ya kupotea kwa watu wenye
ulemavu wa ngozi” alifafanua Mhe. Silima
“kesi 46 kati ya matukio 56 zilifikishwa Mahakamani ambapo kesi 10
zenye watuhumiwa 12 zilitolewa hukumu ya kifo na kumi ziko chini ya upelelezi.
Aidha kesi 26 watuhumiwa wake waliachiwa huru kwa kukosa ushahidi” aliongezea
Mhe. Silima
Kuchelewa kwa hukumu au upelelezi wa baadhi ya kesi zilizotajwa
kunachangiwa na sababu mbalimbali kama vile matokeo ya uchunguzi wa DNA toka
Mamlaka ya Uchunguzi na/au mashahidi kutopatikana kwa urahisi na kwa wakati.
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
0 comments:
Post a Comment