Home » » Wanawake wagombea waweka mikakati ya kushinda udiwani na ubunge 2015

Wanawake wagombea waweka mikakati ya kushinda udiwani na ubunge 2015

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mgeni rasmi wa katika Kongamano hilo Mhe. Getrude Mongella akiwa na baadhi ya wabunge wanawake wa bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania wakiimba nyimbo mbalimbali.



Kwa Mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012, Idadi ya Watanzania sasa imefikia milioni 44.9 huku wanawake wakiwa ni asilimia 51.3 ilihali wanaume ni asilimia 48.7. Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya Mwaka 1977 inabainisha kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni ya kidemokrasia, ya kidunia ambayo inaendeshwa kwa misingi ya kidemokrasia na haki ya kijamii. Ibara ya 8 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatamka wazi kwamba nchi hii ni nchi ya kidemokrasia na haki za kijamii.

Akidi nzima ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni Wabunge 357 kwa mujibu wa Katiba. Hata  hivyo viti maalum pekee ni 102 (28.6%) vilivyogawanywa miongoni mwa vyama vya siasa kwa kuzingatia matokeo yao ya uchaguzi, kati ya viti 239 vya majimbo (vikiwemo kutoka Zanzibar),  ni wanawake 21 tu (8.8%) ndio walipata viti vya kuchaguliwa bungeni. Idadi ya madiwani wa kuchaguliwa asilimia 4, Wenyeviti wa Vijiji Asilimia 2, Wenyeviti wa Mitaa ni asilimia 12  wakati Wenyeviti wa Vitongoji ni asilimia 3tu!!.

Pengo hili la ushiriki wa Wanawake katika nafasi za uongozi zimepelekea asasi za kiraia kuendeleza harakati za kudai ushirikishwaji sawa au usawa katika vyombo vya uawakilishi kati ya Wanawake  na wanaume. Kama sehemu ya kuendeleza mapamabno ya kudai ushiriki wa Wanawake kwenye uongozi, ActionAid Tanzania kwa kushirikiana na TGNP Mtandao waliandaa Kongamano la Wanawake wagombea kwa nafasi zote za uongozi katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu 2015 kuanzia tarehe 14 hadi 15 Juni 2015 lililofanyika mjini Dodoma, ambapo wagombea Wanawake, vijana na watu wanaoishi na ulemavu zaidi ya 200 walikutana na kujadiliana kwa pamoja changamoto wanazokumbana nazo katika harakati za kutafuta ushindi. Waliokutana ni Wanawake , vijana na walemavu walioonesha nia ya kuomba ridhaa ya vyama vyao ili wawe viongozi.

Katika kongamano hilo la aina yake  viongozi/wabunge na viongozi  wastaafu Wanawake ambao wamekuwa madarakani kwa muda mrefu na kupambana na changamoto mbalimbali ambazo zinawakabili Wanawake katika nafasi za uongozi waliweza kushiriki na kutoa  ushauri kwa waonesha nia hao.

Akizungumza katika Kongamano hilo, Meneja wa Haki za Wanawake kutoka ActionAid  Scholasitica Haule alisema jinsi mchakato ulivyo na kasi kubwa ni lazima makundi yote yawe makini na vyama vya siasa navyo viangalie nyuma ili kuhakikisha kila anayestahili kuwa kwenye kasi ya mchakato anapata nafasi.

 “tunajua mchakato wa uchaguzi mkuu unakwenda kwa kasi sasa, tunavitaka Vyama vya siasa vioneshe kwa vitendo nia ya kujenga demokrasia ya ushindani kwanza kwa kuonesha mabadiliko ndani ya uongozi wa vyama. Vyama vya siasa sharti viwe mstari wa mbele kwenye kuonesha kwa vitendo dhana wanazosimamia, kama vile demokrasia, utawala bora na wa sheria. Kwa mantiki hii, sharti mifumo iliyoko ndani ya vyama pamoja na taratibu zake zijengeke kwenye misingi shirikishi, ya kidemokrasia isiyowabagua wanawake au makundi mengine yaliyoko pembezoni” alisema Haule

Naye Mkuu wa wilaya ya Chamwino Farida Mgomi, aliyekuwa mgeni wa heshima katika ufunguzi wa Kongamano hilo, aliwataka  Wanawake walionesha nia ya kugombea uongozi kutokukata tamaa wala kuogopa.

“msiogope, masikate tamaa, simameni imara  ili kuhakikisha mnashinda, wanawake walipata fursa wamefanya vizuri na sote tumneona,  na hata wao ukiwauliza wanakuambia kwamba wamekumbana na changamoto nyingi lakini wamefanikiwa, jambo la msingi ni kuwa na msimamo, kutaa kwa dhati rushwa,  matumizi makubwa ya fedha kwenye uchaguzi ili mnakundi yote  hasa wanawake, vijana na wanaoishi na ulemavu waweze kushiriki na kufanikiwa” alisema DC Mgomi.

Alieleza kwamba Ili kuwapa fursa wanawake, vijana na watu wanaoishi na ulemavu washinde katika uchaguzi huu ni lazima Jamii nzima iunganishe nguvu katika kudai vyama vya siasa vizingatie usawa wa kijinsia katika kupendekeza majina ya wagombea, kuwawezesha kifedha na kuwaunga mkono ili washinde.

Pia Mkuu huyo wa wilaya alivitaka Vyama vya siasa vitoe fursa za pekee kwa wagombea wanawake katika kutumia vyombo vya habari vyote  kutangaza habari za uchaguzi kwa kuzingatia usawa wa kijinsia bila kujali itikadi na kuweka taratibu za kuwezesha watu wenye ulemavu washiriki kikamilifu katika uchaguzi kama wapiga kura na kama wagombea uongozi katika nyadhifa mbalimbali.

Balozi Mstaafu na aliyekuwa Rais wa Bunge la Afrika Dk. Getrude Mongela ambaye aliwafunda Wanawake hao namna ya kuwa viongozi bora na mbinu za kushinda uchaguzi alisema kwamba,  Wanawake wanatakia kujenga hoja na kubeba ajenda za msingi za wananchi wote bila kuwabagua na sio kushambulia wanasiasa wengine majukaani.

Aidha Mongela aliwataka Wanawake kuhakikisha kwamba wao wenyewe wanaunganisha nguvu bila kujali itikadi zao za kichama, kuvua tofauti zao wanapokutana ili kuwa na ajenda moya ya kuhakikisha Wanawake wenye uwezo wanashinda na wanabeba ajenda ya wananchi wote.

“Tukishaanza mipango ya kujigawa kwa itikadi zetu, hatuwezi kushinda, ninawataka  kuunganisha nguvu pamoja na kuhamkikisha hakuna anayeachwa nyuma, lakini tusijenge chuki za kivyama, achana na chama, sema ni mwanamke kwanza, halafu mengine ya vyama yatakuja baadaye, hapo tutaona mabadiliko” alisema Dk. Mongela

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa