Home » » VURUGU KUBWA

VURUGU KUBWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mbowe azingirwa
VURUGU kubwa jana zimeibuka bungeni baada ya wabunge wa kambi ya upinzani kuendelea kushikilia msimamo wao wa kutaka kauli ya Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Nape Nnauye kuhusu kutorushwa moja kwa moja kwa matangazo ya Bunge ijadiliwe.
Mapema jana asubuhi Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge aliahirisha kikao hicho baada ya kuona wabunge wa upinzani wakianzisha vurugu wakati wakipinga kauli hiyo ya Serikali.
Vurugu hizo ziliibuka tena wakati Bunge liliporejea saa 10 alasiri ambapo Mwenyekiti Chenge alikaa kimya kwa takriban dakika 10 hadi Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu alipoomba mwongozo wa mwenyekiti kukaa kimya.
Chenge alisimama na kutoa taarifa ya Kamati ya Uongozi, akisema mambo matatu ndiyo yaliyoamuliwa.
“Kamati ya Uongozi imeamua mambo yafuatayo, kwanza Mwenyekiti alikuwa sahihi kukataa kukatisha mjadala wa hotuba ya rais. Kuhusu kanuni ya 51, hakuna kanuni yoyote iliyovunjwa hasa ile ya Haki, Hadhi na Madaraka ya Bunge,” alisema Chenge na kuongeza:
“Hoja iliyo mbele yetu yaani hotuba ya rais iendelee na endapo kuna mbunge yeyote ambaye hataridhika na hatua hiyo, atumie kanuni ya nne fasiri ya tano kuwasilisha malalamiko yake.”
Baada ya Chenge kutoa maelezo hayo na kumwalika mbunge aliyetakiwa kuchangia, Lissu aliinuka na kuomba mwongozo akisema haikuwa sahihi kwa mwenyekiti kupeleka tatizo hilo kwenye Kamati ya Uongozi badala ya Kamati ya Kanuni.
“Ni sahihi kwa masuala ya kanuni kupelekwa kwenye Kamati ya Uongozi badala ya Kamati ya Kanuni? Pili, kwanini mwenyekiti unakaimisha mamlaka ya kiti chako kwenye Kamati ya Uongozi? Naomba mwongozo wako,” alisema Lissu.
Akijibu mwongozo huo, Chenge alisema ametumia busara ya kawaida kumtaka Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe alete hoja yake.
“‘No any monopoly and I am very open’, someni kanuni,” alisema Chenge.
Baada ya hapo alimkaribisha katibu ili ataje utaratibu, naye akasema ni kuendelea kwa mjadala. Lakini wabunge wa upinzani waliendelea kuomba mwongozo.
Mbunge wa Babati Mjini, Paulina Gekul, alisimama na kuomba mwongozo jambo lililomkera Chenge, hata hivyo alimruhusu.
Gekul alitaja kanuni ya 49 akisema kauli za mawaziri hazipaswi kuzua mjadala.
“Kauli ya waziri imezua mjadala kwanini unatukataza kuijadili wakati kanuni zimeruhusu?” alihoji Gekul.
Naye Mbunge wa Tarime, John Heche, aliomba mwongozo na kusema kauli ya Waziri Nape imekwenda kinyume na Katiba ibara ya 18 (d).
“Tuko hapa kujadili mambo muhimu, wananchi wana haki ya kupata taarifa. Tutakuwa watu wa ajabu kuvunja Katiba,” alisema Heche.
Alipomaliza wabunge wote wa upinzani walisimama wakitaka mwongozo.
Chenge alijaribu kuwasihi wabunge hao wakae, lakini waligoma.
Aliwaambia kama hawajaridhika wafuate kanuni.
Wakati huo, baadhi ya wabunge wa CCM walikuwa wakipiga kelele, “toa nje haoooo”.
Chenge aliwaambia wabunge wa upinzani kuwa kama hawataki huo mjadala watoke nje. Wakati huo pia mmoja wa wasaidizi wa Katibu wa Bunge alimpa Chenge orodha ya majina aliyosema watoke nje.
Aliwataja wabunge hao kuwa ni  Tundu Lissu, Esther Bulaya, Godbless Lema na Paulina Gekul. Lakini waligoma.
Lema aliinuka na kusema “Wataniua hapa siondoki,” huku wabunge wa upinzani wakishangilia. Ndipo Chenge alipoagiza wabunge wote wa upinzani watoke nje.
“Naahirisha shughuli za Bunge kwa dakika 10 ili polisi wafanye kazi yao,” alisema Chenge na kutoka nje ya Bunge.
Wakati huo, baadhi ya askari wa Bunge walifika na kuwasihi wabunge wa upinzani watoke nje nao wakagoma.

LIJUALIKALI ABURUZWA 
FFU WAWADHIBITI UKAWA.
Ghafla askari wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU) waliingia ndani ya ukumbi wa Bunge na kuwazunguka wabunge wa upinzani.
Askari hao walijaribu kila namna, lakini walishindwa kuwatoa.
Ilichukua takriban nusu saa kuwalazimisha wabunge hao kutoka nje. Mwishowe askari hao walianza kumtoa mmoja mmoja kwa nguvu.
Baadhi ya wabunge wakiwemo, Susan Kiwanga wa Kilombero na Halima Mdee wa Kawe waliburutwa kwa nguvu na askari hao.

WAANDISHI WANYANG’ANYWA SIMU, KAMERA

Wakati vurugu hizo zikiendelea, Mkuu wa Idara ya Habari na Uhusiano bungeni, Owen Mwandumbya, akiwa na maofisa wenzake waliwaondoa waandishi wa habari kwenye vyumba vyao na kuwapiga marufuku wapigapicha kuchukua matukio yaliyokuwa yakiendelea bungeni.
Hata waandishi wa habari walipotoka nje, maofisa usalama waliwazuia kuandika kitu chochote wala kupiga picha nje ya maeneo ya Bunge kabla ya kuruhusiwa kuingia tena ndani, lakini hawakutakiwa kufanya kazi nje ya Bunge na wengine wakinyang’anywa simu, kamera na vifaa vingine na kutakiwa kufuta picha walizozipiga katika tukio hilo.
CHANZO; MTANZANIA.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa