Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MWANASHERIA Mkuu wa Serikali, George Masaju amewataka wabunge
kusimamia utekelezaji wa sheria wanazotunga na si kuhamasisha uvunjaji
wa sheria za nchi. Alitoa kauli hiyo jana wakati akijibu swali la
nyongeza la Mbunge wa Konde, Khatib Said Haji (CUF).
Mbunge huyo alihoji kwa nini serikali haiwachukulii hatua watu
wanaofanya uhalifu Zanzibar na kama wameshindwa, wananchi wawaadhibu
wahalifu hao kwa kuwapiga mawe? Pia Mbunge huyo alitaka Waziri wa Mambo
ya Ndani atamke kama wameshindwa kudhibiti uhalifu huo, wananchi
washughulikie wahalifu hao kwa kuwapiga mawe na magari yao.
Akijibu swali hilo mwanasheria mkuu wa serikali, alisema hoja ya
Mbunge huyo sio sahihi na kusisitiza, “Waziri hawezi kutamka watu
wavunje sheria, wabunge wanatunga sheria wanatakiwa kusimamia
utekelezaji wake”.
Kwa upande wake, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala
Bora, Angelah Kairuki alisema kuhusiana na hoja kuwa vyombo vya dola
vinakiuka haki za binadamu, endapo mbunge huyo ana malalamiko awasilishe
kwenye tume ya haki za binadamu ili yapate kushughulikiwa.
Mbunge wa Rombo, Joseph Selesini (Chadema) katika swali la nyongeza
alihoji kwa kuwa matukio ya wananchi kuchukua sheria mkononi
yanasababishwa na mambo mawili, ikiwemo polisi kwenda kwenye tukio
wakiwa wamechelewa na wahalifu wanapokamatwa baada ya muda wanaachiwa.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad
Yusuf Masauni alisema Jeshi la polisi linajitahidi kufanya kazi, idadi
ya polisi haitoshelezi kutokana na polisi mmoja kuhudumia watu 300 hadi
350.
“Wakati mwingine inatokea baadhi ya polisi wana mapungufu na wamekuwa
wakichukuliwa hatua za kisheria na wale wanaotenda makosa ya jinai
sheria imekuwa ikifuata mkondo wake,” alisema.
Katika swali la msingi,Mbunge huyo wa Konde alihoji juu ya matukio ya
wananchi kujichukulia sheria mkononi yamezidi kuongezeka na kusababisha
madhara na vifo kwa watu wasio na hatia.
Akijibu swali hilo, Masauni alisema vitendo vya mtu au watu
kujichukulia sheria mkononi ni uhalifu ambao umeanza kushamiri katika
jamii ikiwemo visiwa vya Zanzibar. Alisema katika kipindi cha mwaka
2013/2014 jumla ya matukio 2,041 yaliripotiwa katika vituo mbalimbali
vya polisi nchini.
Mwaka 2013 kulikuwa na matukio 1,112 ambapo Zanzibar yaliripotiwa 14
na mwaka 2014 yalipungua na kufikia matukio 929, kati ya hayo watuhumiwa
walichukuliwa hatua stahiki ikiwemo kufikishwa mahakamani.
CHANZO : HABARI LEO.
0 comments:
Post a Comment