Home » » KAIRUKI KUTUMBUA MAJIPU FEDHA ZA TASAF III

KAIRUKI KUTUMBUA MAJIPU FEDHA ZA TASAF III

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), Angela Kairuki.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), Angela Kairuki, amesema atawachukulia hatua viongozi waliotumia vibaya fedha za Mpango wa Kunusura Kaya Masikini unaosimamiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Awamu ya Pili (Tasaf III).
 
Alisema hayo wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Bunda (Chadema), Ester Bulaya, aliyehoji fedha za Tasaf III zimekuwa zikitumiwa vibaya na kwamba kuna mgombea urais uchaguzi mkuu uliopita alitumia fedha za hizo kufanyia kampeni.
 
Kairuki alisema amepata malalamiko hayo na kwamba anayafanyia kazi ili kuwabaini waliohusika na suala hilo.
 
Alisema atawachukulia hatua kwani fedha za Tasaf zinatakiwa kutumika kwa malengo yaliyowekwa na siyo vinginevyo.
 
Awali akijibu swali la msingi la Mbunge wa Kaliua, Magdalena Sakaya (CUF), Kairuki alisema asilimia 30 ya vijiji na mitaa katika halmashauri zote imepangwa kufikiwa na mpango huo mwaka huu.
 
Alisema vijiji 54 sawa na asilimia 70 ya vijiji vyote katika wilaya ya Kaliua, mkoa wa Tabora viko katika mpango wa tatu wa kunusuru kaya masikini (TASAF III).
 
 “Serikali ilitoa maagizo ili kufikia vijiji, mitaa na shehia zote zilizobaki. Vilivyoanza ndiyo nvilikuwa na hali mbaya zaidi,” alisema.
 
Kairuki mpango huo hutambulishwa kijijini na wataalam kutoka halmashauri husika kwa kusimamiwa na uongozi wa kijiji, kisha kuweka vigezo vya kaya masikini.
 
“Wakusanya taarifa huchaguliwa kutoka miongoni mwa vijana wanaoishi kijijini hapo ambao hupita nyumba kwa nyumba kuorodhesha kaya zinazokidhi vigezo vilivyoainishwa na mkutano mkuu wa kijiji,” alisema.
 
Alisema orodha ya kaya zilizoorodheshwa na timu ya wakusanya taarifa husomwa mbele ya mkutano wa kijiji na kisha majina kujadiliwa.
 
“Kutokana na orodha hiyo, kaya hizo hujaziwa dodoso maalum linaloandaliwa na TASAF makao makuu kwa lengo la kupata taarifa zaidi za kaya. Dodoso hilo huchambuliwa kupitia mfumo maalum wa kompyuta ili kupata kaya masikini sana zinazokidhi vigezo,” alisema Kairuki.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa