Home » » MPANGO MPYA WA UMEME VIJIJINI KUSUBIRI.

MPANGO MPYA WA UMEME VIJIJINI KUSUBIRI.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
WAZIRI wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amesema Awamu ya Tatu ya mpango wa kusambaza umeme vijijini unaotekelezwa na Wakala wa Umeme Vijijini (REA) hautaanza mpaka kukamilika kwa miradi ya awamu ya pili na ya kwanza.
Alisema hayo bungeni juzi wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Mkalama, Allan Kiula (CCM) aliyetaka kufahamu lini vijiji vilivyo katika jimbo lake vitapata umeme kutokana na miradi ya REA inayoendelea.
Profesa Muhongo alisema Februari 6 na 7, mwaka huu watafanya mkutano wa tathmini ya miradi inayotekelezwa na REA awamu zote. “Tunataka kujua makandarasi waliopo kazini, malipo waliyopewa kama yanalingana na kazi wanazofanya na je kazi zinaendeleaje,” alisema.
Alisema baada ya mkutano huo akishirikiana na Naibu Waziri na makatibu wakuu wa wizara hiyo watakwenda nchi nzima ili kuangalia kitu gani kinachoendelea.
Katika swali la msingi, Mbunge wa Makambako, Deo Sanga (CCM) alitaka kufahamu lini miradi ya umeme itakamilika katika vijiji vya Mawande, Utengule, Luhota, Ngamanga, Ikwata, Mlowa, Mkolonga, Ibumila, Mahongole, Manga Usetule, Kifumbe, Mtanga, Kitandililo, Ibatu, Nyamande Mtulingala na Mbugani.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk Medard Kalemani alisema Serikali imeweka mkandarasi Lucky Exports ambaye kwa sasa anatekeleza mradi wa REA awamu ya pili mkoani Njombe.
Alisema kazi ya usanifu imekamilika kwa sasa na mkandarasi anasubiri kusaini mkataba kati yake na REA kabla ya Machi, 2016 ili aanze utekelezaji wa mradi katika vijiji vya Ikwete, Kifumbe, Luhota, Manga, Mlowa, Mwande, Ngamanga, Usetule na Utengule.
Alisema kazi hiyo itachukua miezi sita na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,875, mpaka kukamilika kwake kazi hiyo itagharimu Sh bilioni 3.3 na vijiji vya Mahongole, Manga, Mbugani, Mtanga, Mtulingala na Nyamande vimewekwa kwenye mradi awamu ya tatu.
CHANZO ; HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa