Home » » UJENZI RELI YA KATI YA KISASA WATAWALA BUNGE.

UJENZI RELI YA KATI YA KISASA WATAWALA BUNGE.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
UJENZI wa Reli ya Kati ya kisasa umetawala mjadala bungeni huku wabunge wengi wakiitaka serikali kuhakikisha bajeti ijayo, inakuja na majibu juu ya hilo. Wabunge wengi waliochangia mpango wa Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/17 juzi na jana, walitaka serikali ioneshe kwamba ujenzi huo utaanza mara moja katika mwaka ujao wa fedha.
Mbunge wa Kigamboni, Faustine Ndugulile (CCM) alihimiza serikali kuweka kipaumbele cha ujenzi kwa ajili ya kuinua uchumi. Mbunge wa Viti Maalumu, Mwanne Nchemba (CCM) pia alisisitiza akisema, “Serikali isidharau kwa sababu reli ni tegemeo kubwa kwa wananchi na pia kwa ubebaji wa mizigo.”
Akizungumzia gharama kubwa za ujenzi, Mbunge wa Kasulu Mjini, Daniel Nsazugwanko (CCM), alishauri serikali isiogope kukopa. “Hoja kwamba hakuna fedha, hatutaki kuisikia badala yake serikali ije na mkakati wa makusudi...bila kuwa na reli tunacheza ngoma,” alisema.
Nsazugwanko aliendelea kusema, “Waziri usipokuja na mkakati wa kujenga Reli ya Kati, hatuwezi kuelewana bungeni.” Aliwataka wabunge wote kusimama kidete juu ya suala hilo.
Alitoa mfano wa Kenya kwamba wameanza kujenga reli ya Mombasa kwenda Kigali huku akisisitiza pia serikali ihakikishe inajenga reli pia kwenye michepuko kuelekea maeneo yenye rasilimali, kama vile madini Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Alisema bila kujenga Reli ya Kati kwa kiwango cha kisasa, pia bandari za Dar es Salaam, Mwanza, Kigoma na Kalema zitadorora. “Tutashawishiana wabunge wote tuombe uje tena... bila Reli ya Kati, hakuna viwanda,” alisisitiza.
Mbunge wa Kigoma Mjini, Kabwe Zitto alisisitiza umuhimu wa ujenzi wa reli na kuitaka serikali kuwa makini kwenye siasa za kikanda kwa kuhakikisha mtandao wa reli unakamilika. Alitaka pia wapate tafsiri ya Reli ya Kati kwa maana ya matawi yake, na kuongeza kuwa mwaka jana ilianzishwa kodi ya maendeleo ya reli ambayo kila mzigo unaoingia nchini unatozwa asilimia 1.5 ya maendeleo ya reli.
Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Peter Serukamba (CCM) alimtaka Waziri mwenye dhamana ataje Reli ya Kati inayolengwa kujengwa, ihusishe matawi ya Kaliua-Mpanda-Kalema; Uvinza- Msongati; Isaka-Keza. “Suala la reli ni la kufa na kupona,” alisema.
Wakichangia maeneo mengine, Mbunge wa Kigamboni, Ndugulile alishauri Bandari ya Dar es Salaam ipanuliwe na ifanye kazi kwa saa 24 huku akisisitiza ushirikishaji wa sekta binafsi katika miradi ya maendeleo.
Kwa upande wa maji, alishauri kuwe na mpango kama wa Wakala wa Umeme Vijijini (REA) kwa ajili ya kuwezesha huduma vijijini na uwepo mfuko kwa ajili ya maji kama ilivyo kwa barabara.
Vile vile katika michango ya wabunge wengi, walishauri uanzishaji viwanda uendane na jiografia ya maeneo husika sanjari na rasilimali zinazopatikana. Kwa upande wa usafiri wa anga na ununuzi, Zitto alisema serikali haiwezekani ikawa inanunua ndege kila wakati.
Alishauri taasisi na watu wanaonufaika na kuwepo kwa ATCL, ambazo ni pamoja na TANAPA na Ngorongoro, ziruhusiwe kuwa na hisa kwenye shirika hilo la ndege. Akizungumzia ahadi ya Sh milioni 50 kwa kila kijiji, Zitto alishauri zitumike kutoa motisha wananchi wengi wajiunge na huduma ya hifadhi ya jamii.
Aidha, Mbunge wa Babati Mjini, Pauline Gekul (Chadema) alipinga mapendekezo ya kutaka Mamlaka za Serikali za Mitaa, kuwasilisha mapato yao kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali kwa kile alichosema kutaua halmashauri.
CHANZO ; HABARI LEO.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa