Home » » Askofu: Magufuli tumemkubali, tunamuombea

Askofu: Magufuli tumemkubali, tunamuombea

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Askofu Mkuu wa Kanisa la TAG, Dk Barnabas Mtokambali
ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God (TAG), Dk Barnabas Mtokambali amesema Mungu ameikumbuka Tanzania kwa kuipatia kiongozi mkuu wa nchi mwenye uchungu na taifa lake.
Dk Mtokambali amemtaja Magufuli kuwa ni miongoni mwa viongozi wachache Afrika wenye malengo na nchi, ambao hutokea kwa nadra.
Alimfananisha na viongozi kama Mwalimu Julius Nyerere, Patrice Lumumba wa Kongo na Kwame Nkrumah wa Ghana. Askofu Mtokambali alisema hayo juzi wakati wa sherehe ya kuweka wakfu jengo jipya la kanisa la TAG Nkuhungu.
Alisisitiza kwamba kanisa linasimama na serikali iliyopo madarakani.
“Magufuli tumemkubali, wanyang’anyi, wala rushwa, wezi hawatampenda, kanisa tunampenda, tunamkubali na tunamuombea. Ni nadra kupata rais mwenye mzigo na nchi, hutokea mara chache sana,” alisema.
Alisema rais amekuwa na maadui wengi kutokana na kugusa maslahi ya watu. Wakati huo huo, akizungumzia kanisa hilo, alisema limefanikiwa kuchimba visima 30 na vyote vinafanya kazi .
Alisema pia wamezindua zahanati bora katika mji wa Dodoma na sasa wana mkakati wa kufanya kiwe kituo cha afya. Akizungumzia elimu, alisema kanisa hilo lina mpango wa kujenga chuo kikuu kikubwa katika eneo la Chigongwe na wamefuata taratibu zote za serikali .
Kwa mujibu wa askofu mkuu, wana eneo la ekari 560. Pia ekari 100 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za watumishi watakaofanya kazi chuoni hapo. Alisema changamoto kubwa iliyotokea ni baadhi ya watu kujitokeza na kudai maeneo hayo kuwa ni yao.
Hata hivyo, alisema walishinda kesi hiyo mara mbili, lakini mpaka sasa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) haijafanya utekelezaji mpaka sasa.
“Miaka minane sasa CDA wamebaki kimya, wamekuwa kikwazo cha ujenzi wa chuo, serikali itusaidie katika hili,” alisema. Kwa upande wake, Askofu wa TAG Kanda ya Dodoma, Steven Mahinyila alisema ujenzi huo ulianza mwaka 2011.
Alisema ulikwama kutokana na ukosefu wa fedha na ndipo mwaka jana walipata msaada kutoka kwa kampuni ya Priority One ya Marekani, ambayo ilitoa fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi huo.
Chanzo Kutoka Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa