Home » » DC Mpwapwa aikumbusha halmashauri

DC Mpwapwa aikumbusha halmashauri

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Imeandikwa na Sifa Lubasi, Mpwapwa.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Jordan Rugimbana.
HALMASHAURI ya wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma imetakiwa kutenga asilimia 10 ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya akinamama na vijana na kuhakikisha zinawafikia walengwa.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Mohamedi Utaly wakati akizungumza na vikundi vya wajasiriamali kwenye kongamano la wajasiriamali lililofanyika juzi katika Ukumbi wa Chuo cha Ualimu Mpwapwa.
Utaly alisema halmashauri itenge asilimia 10 ya mapato yake ya ndani kwa lengo la kupunguza na kuviwezesha vikundi vya akinamama na vijana ili kujikwamua na umasikini wa kipato na kuwezesha vikundi hivyo kumiliki mali.
Pia aliitaka halmashauri hiyo kutenga maeneo ya wajasiriamali hao, kuzifanyia maonesho bidhaa wanazozalisha kwa kujitangaza zaidi kuinua uchumi wao binafsi na uchumi wa wilaya nzima.
Katibu wa maandalizi wa kongamano hilo, Mary Luambano alisema lengo la tamasha hilo ni kuviwesha vikundi vya akinamama na vijana kutumia fursa zinazowazunguka kujipatia kipato na kuinua maisha ya kila siku na jamii kwa ujumla lakini pia kuzitumia taasisi za kifedha katika kujipatia mikopo yenye masharti nafuu.
Luambano alisema wajasiriamali wengi wamekuwa wakishindwa kufikia malengo yao ya kuanzisha biashara kubwa kutokana na changamoto zinazowakabili kwa kukosekana kwa mpango kamili wa uwekaji akiba, elimu ndogo ya ujasiriamali na mazingira rafiki ya kufanyia biashara hizo.
Alisema kumekuwa na changamoto kubwa ya wajasiriamali wengi juu ya mikopo wanayoipokea kutokuwa msaada kwao baadhi yao mikopo hiyo imekuwa chanzo cha kuwarudisha nyuma na kufilisika kabisa kutokana na kutumia fedha ya mkopo vibaya lakini riba kubwa zinazotozwa na tasisi za kifedha kwa wajasiriamali.
Mwalimu wa vikundi vya ujasiriamali ambavyo vipo chini ya Mradi wa Tunajali, Erasto Dyamaza alisema mpaka sasa vikundi vya hisa vina mtaji wa kiasi cha Sh milioni 131.
Alisema kuna ulazima kwa serikali katika mipango yake izingatie mahitaji muhimu ya kijinsia kama zinavyotaka sera na mikataba mbalimbali ya kimataifa ikiwa katika malengo makuu ya kufanya maamuzi, udhibiti wa rasilimali, uhakika wa kupata chakula, ukatili wa kijinsia na mirathi.
Chanzo Gazeti la Habari Leo
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa