Home » » MAADHIMISHO SIKU YA WAUGUZI DUNIANI WILAYANI CHAMWINO YAFANA

MAADHIMISHO SIKU YA WAUGUZI DUNIANI WILAYANI CHAMWINO YAFANA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa, Mhe. George Lubeleje akiwahutubia Wauguzi wa Hospitali Teule ya Mvumi, Wilayani Chamwino Mkoani Dodoma 14 Mei, 2016 wakati wa wakiadhimisha Siku ya Wauguzi Duniani.


Na Benedict Liwenga, Dodoma.


Wauguzi Wilayani Chamwino pamoja na wengineo nchini wamepewa pongezi kwa mchango wao mkubwa wanaoutoa wa kutoa huduma ya afya kwa jamii ikiwemo kuendeleza huduma hiyo nchini.


Pongezi hizo zimetolewa na Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa, Mhe. George Lubeleje katika Hospitali Teule ya Mvumi iliyopo Wilayani Chamwino mkoani Dodoma  wakati alipomwakilisha Spika wa Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania, Mhe. Job Ndugai ambaye alikuwa mgeni rasmi katika Maadhimisho ya Siku ya Wauguzi Duniani.


Mhe. Lubeleje amesema kuwa bila kuwepo kwa wauguzi huduma ya afya ingeyumba kutokana na ukweli kwamba Wauguzi hao ni zaidi ya asilimia 60 ya Watumishi wote wa sekta ya afya ambapo wanatekeleza asilimia 80 ya shughuli zote za afya.


Amefafanua kuwa, Wauguzi ndiyo wenye kuandaa mazingira mazuri kwa daktari kutekeleza majukumu yake kwani baada ya daktari kumaliza kumuona mgonjwa na kutoa maelekezo yake, muuguzi husimamia utekelezaji wa maelekezo hayo pamoja na tiba na huduma kwa mgonjwa husika.


Ameongeza kuwa, mara nyingi muuguzi ndiye anayefanya kazi ya kuuguza mgonjwa kwani wagonjwa wengi hutumia muda mwingi wakiwa mikononi mwa wauguzi kuliko wanaoutumia mikononi mwa wahudumua wengine wa sekta ya afya.


Aidha, Mhe. Lubeleji amewapongeza wauguzi hao kutokana na kaulimbiu yao katika Maadhimisho ya Wauguzi Duniani isemayo “Wauguzi; Nguvu ya Mabadiliko: Uboreshaji wa uthabiti wa mifiumo ya afya” ambapo amesema kwamba ni kaulimbiu katika wakati muafaka kwakuwa wauguzi wana nafasi maalum katika maendeleo ya huduma ya afya na sekta yenyewe kwa ujumla.


“Ni chachu muhimu ya mabadiliko katika sekta ya afya, na ndiyo rasilimali ya kuwawezesha uboreshaji wa uthabiti wa mifumo ya afya”, alisema Mhe. Lubeleje.


Akifafanua baadhi ya changamoto zinazoikabili Hospitali Teule ya Mvumi wilayani hapo, alisema kuwa Serikali inaelewa kuhusu mchango wa wauguzi na inauthamini kwa kiasi kikubwa, vile vile amewahakikishia wauguzi hao kuwa Serikali imekuwa ikijitahidi kuboresha maslahi ya Watumishi wa Umma wakiwemo wa afya, hususani katika masuala ya mishahara na posho mbalimbali.


“Maombi yenu nimeyapokea na ninaahidi nitayawasilisha kwenye Mamlaka husika kwa ajili ya utekelezaji, yale yanayotuhusu, kama Bunge tutayachukua pia na kuisimamia Serikali ili iyatekeleze na hatimaye tuimarishe huduma za uuguzi na afya kwa ujumla”, alisema Mhe. Lubeleje.


Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Chamwino, Mhe. Farida Mgomi amewasisitiza Wauguzi wilayani hapo kujituma kwa bidii katika kutekeleza majukumu yao ya kutoa huduma ya afya kwa jamii kwani Serikali ya Awamu ya Tano inahitaji mabadiliko yanayoendana na kasi ya “Hapa Kazi tu” kwa kuwahudumia wananchi nchini.


Aidha, amewapongeza kwa juhudi zao na maarifa katika kazi yao na kuwahakikishia kuwa Serikali itazidi kushirikiana nao katika kuleta maendeleo katika sekta hiyo na kusimamia vema katika masuala yao mbalimbali.


Sikua ya Wauguzi Duniani huadhimishwa tarehe 12 Mei kila mwaka ikiwa ni kumbukumbu ya kuzaliwa kwa Mwanzilishi wa Uuguzi Bi. Florence Nightngale aliyezaliwa tarehe 12 Mei, 1820 na kufariki mwaka 1910.


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa