Maadili ni Msingi wa Uwajibikaji katika Utumishi wa Umma
Anitha Jonas - MAELEZO
TANGU
enzi za Azimio la Arusha, suala la maadili limekuwa likisisitizwa kama
nguzo muhimu katika utoaji wa huduma kwa umma. Lengo lilikuwa ni
kuhakakisha kwamba kila mtumishi wa Umma anatekeleza wajibu wake kwa
kufuata sheria, kanuni na miongozo iliyowekwa.
Kutofanikiwa
kwa Azimio la Arusha kulitokana na baadhi ya Viongozi kujua kwamba
utekelezaji wa malengo ya azimio hilo ungekwamisha nia ovu
waliyokuwanayo kama Watumishi wa Umma katika kuwahudumia Wananchi. Ndio
maana juhudi ya Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere za
kutaka azimio hilo liungwe mkono hazikuzaa matunda.
Pamoja
na kuwepo sheria, kanuni, miongozo na mikakati ya kukuza maadili kwa
watumishi wa Sekta ya Umma na watu binafsi, wananchi bado wamekuwa
wakilalamika kuwepo urasimu usio wa lazima wenye lengo la kutengeneza
mazingira ya rushwa na huduma zisizoridhisha. Aidha, wapo baadhi ya
wafanyabishara binafsi wasiozingatia maadili na hata kufikia hatua ya
kuchochea utoaji wa rushwa au kuzalisha bidhaa zisizo na viwango.
Katika
jitihada za kuhakikisha kwamba watumishi wa Umma wanakuwa waadilifu na
wanafuata maadili mema, Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Mstaafu
Dkt. Jakaya Kikwete ilibuni mikakati ya kuwa na utaratibu mpya kwa
viongozi na watumishi wa Sekta za Umma na Binafsi kusaini Ahadi ya
Uadilifu (integrity pledge).
Ahadi
ya Uadilifu ni tamko rasmi na bayana la dhamira ya kuwa na mwenendo wa
kimaadili na kuunga mkono kampeni ya kitaifa ya maadili na mapambano
dhidi ya rushwa. Kwa kusaini tamko hilo, mhusika au taasisi inakuwa
imejipambanua kwa Umma kuwa haitajiingiza katika masuala yasiyo ya
kimaadili katika utoaji huduma na uendeshaji wa biashara.
Kwa
mujibu wa Kamishina wa Maadili Jaji Salome Kaganda, kuna aina tatu za
hati za Ahadi ya Uadilifu yaani; Ahadi ya Uadilifu kwa Viongozi wa Umma,
Watumishi wa Umma na Sekta binafsi ili kila kundi liwajibike kwa namna
yake.
Akizindua
Hati za Uadilifu mwezi agosti 2015, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema,
kuwepo kwa Hati hizo ni hatua kubwa muhimu na ya kihistoria katika
safari ya kuboresha na kuhuisha mifumo ya uadilifu iliyopo ili iweze
kwenda sambamba na mazingira na nyakati zilizopo.
Dkt. Kikwete hakusita kuelezea chimbuko la Hati ya Madili kwa kusema, “Kwa muda mrefu kumekuwepo na changamoto kubwa katika kupambana na rushwa kama moja ya tatizo kubwa la utovu wa uadilifu nchini.
Tumechukua
hatua kadhaa ikiwemo kutengeneza Mkakati wa Mapambano Dhidi ya Rushwa
na mabadiliko katika Sheria ambayo ilisaidia kuanzishwa kwa Taasisi ya
Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU). Tumepata mafanikio makubwa na
ya kutia moyo ingawa bado zipo changamoto na manung’uniko ambayo
hatuwezi kuyapuuza.”
Dkt.
Kikwete alifafanua kuwa, kwa madhumuni ya kuyaongezea mapambano haya
nguvu na kasi, Serikali iliamua Mpango wa Mapambano dhidi ya Rushwa
uingizwe katika Mpango wa Tekeleza kwa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) ili
kutoa msukumo wa pekee katika utekelezaji wake.
Akielezea juu ya Mpango wa Tekeleza kwa Matokeo Makubwa Sasa (BRN), Mkurugenzi Mtendaji wa BRN Bw. Omar Issa alisema
kuwa Ahadi ya Uadilifu ni moja ya maeneo 12 yaliyo katika Mpango wa
Mapambano dhidi ya Rushwa chini ya Mpango wa Tekeleza kwa Matokeo
Makubwa sasa (BRN).
Kwa
mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji huyo, matokeo ya utafiti uliofanywa
katika kutekeleza mpango huo imeonekana kwamba moja ya changamoto
iliyoonekana katika eneo la utoaji huduma na uendeshaji biashara nchini
ni tatizo la rushwa na utovu wa maadili katika taasisi za umma na
binafsi. Hivyo kulikuwa na haja ya kuweka mikakati ya uwajibikali na
kufuata maadili katika utumishi wa Umma na Sekta binafsi.
Katika
kuweka msisistizo wa suala la maadili na uwajibikaji kwa Watumishi wa
Umma, Rais wa Awamu ya Tano Dkt. John Pombe Magufuli ametoa agizo kwa
watumishi wote wa umma kujaza Hati ya Ahadi ya Uadilifu (integrity pledge) ambayo imeeleza wazi masharti ya namna mtumishi wa Umma anavyopaswa kufanya kazi.
Lengo
ni kusaidia kukuza maadili na mapambano dhidi ya vitendo vya rushwa
katika Sekta ya Umma na binafsi kwa kuwa ahadi au tamko hilo
linashawishi viongozi, watumishi wa Umma na Makampuni binafsi kuwa
tayari kufanya kazi kwa kufuata misingi ya maadili na kupambana na
rushwa kwa hiari yao wenyewe.
Akiunga
mkono juhudi za Dkt. Magufuli katika kusimamia nidhamu kwa Watumishi wa
Umma, aliyekuwa Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue amesema kwamba
Hati ya Uadilifu (integrity pledge) itakuwa
chachu ya harakati za kukuza uadilifu na mapambano dhidi ya rushwa
nchini. “Ahadi ya uadilifu itaweka kauli thabiti ya kimaadili ambayo
itaonyesha nia ya kutekeleza majukumu ya viongozi na watumishi wa umma,” alisisitiza Balozi Sefue.
Alifafanua
kuwa, ujazaji wa Hati hiyo hiyo utakuza utamaduni wa viongozi,
watumishi wa Umma na Sekta binafsi kwa ujumla kuwa tayari kufanya kazi
kwa kufuata misingi ya maadili na kupambana na rushwa kwa hiari yao.
Naye
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora Bi. Angela
Kairuki amesema kwamba mtumishi wa umma anatakiwa kufanya kazi kwa
kuzingatia taratibu na uadilifu bila kutoka nje ya mstari.
Mara
baada ya kuapishwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw Agrey Mwanri amesema
atasimamia ipasavyo maadili ya utumishi wa Umma hususan katika
kutekeleza miradi ya maendeleo katika mkoa wake huku akiahidi
kuwawajibisha watumishi watakaokiuka maadili ya utumishi wa umma.
Tangu
achaguliwe kuwa Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, Dkt. John Pombe
Magufuli amewachukulia hatua baadhi ya viongozi wa Umma kwa kushindwa
kusimamia utekelezaji wa majukumu waliyopewa. Viongozi hao ni pamoja na
Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dkt. Shaaban Mwinjaka, Mkurugenzi wa
Mamlaka ya Bandari, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Mapato, Mkurugenzi wa
Vitambulisho vya Taifa na Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana
na Rushwa Dkt.
0 comments:
Post a Comment