Home » » MARUFUKU USAFIRISHAJI WA WANYAMA HAI NJE YA NCHI KWA MIAKA 3.

MARUFUKU USAFIRISHAJI WA WANYAMA HAI NJE YA NCHI KWA MIAKA 3.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Na. Aron Msigwa - Dodoma.
Serikali imesitisha rasmi utoaji wa vibali na uuzaji wa wanyama hai kutoka katika hifadhi za Taifa kwenda nje ya nchi kwa kipindi cha miaka 3 kuanzia Juni 25,2016.
Waziri wa Maliasili na Utalii Prof. Jumanne Maghembe ametoa agizo hilo bungeni mjini Dodoma wakati akijibu hoja na michango mbalimbali ya wabunge iliyoelekezwa kwenye wizara hiyo wakati wa Majumuisho ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hiyo kwa mwaka 2016/2017 ambayo imetengewa kiasi cha  shilingi bilioni 135.7.
Prof. Maghembe ameiagiza Idara ya Wanyamapori ipange na kuweka utaratibu mpya utakaotumika kusimamia biashara hiyo pindi itakaporejeshwa tena baada ya kumalizika kwa muda wa zuio la Serikali la miaka 3, utakaozingatia  mazingira ya uhifadhi wa wanyama hao.

ZUIO LA USAFIRISHAJI WA WANYAMA HAI NJE YA NCHI.
Amesema kumekuwa na taarifa za baadhi ya watanzania wasio waaminifu ambao wamekua wakijihusisha na vitendo vya kusafirisha wanyama hai waliokatazwa kinyume cha utaratibu jambo ambalo limeisababishia Serikali ipoteze mapato kutokana na wanyama hao.
Amesema wanyama wanaoruhusiwa kusafirishwa nje ya nchi kama nyani, Kenge,ndege, kobe, wadudu na tumbili amesema wanyama hao wamekuwa wakisafirishwa  kinyume cha utaratibu na baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu kwa ajili ya kutumiwa na makampuni ya kimataifa kwenye shughuli za utafiti wa kisayansi wa tiba na chanjo.

Aidha, watu na makampuni hayo yamekuwa yakinufaika binafsi kwa kupata fedha nyingi pindi yanapofanikiwa kupata chanjo au tiba husika huku maeneo waliokotoka yakipata fedha kidogo jambo ambalo serikali ya awamu ya tano imeamua kulifanyia kazi.

UTALII KUSINI MWA TANZANIA NA MAENEO MENGINE.
Serikali itatekeleza miradi mbalimbali ya uboreshaji wa Utalii wa Kusini ili kuweka mazingira wezeshi na kuondoa vikwazo vilivyokuwa vikisababisha watalii kushindwa kufika katika maeneo ya hifadhi za Taifa eneo la ukanda wa kusini  mwa Tanzania.
Baadhi ya maeneo yatakayoshughulikiwa ni gharama ya usafiri wa ndege  kwenda na kurudi katika maeneo hayo kuwa kubwa hadi kufikia Dola za kimarekani 1800 jambo ambalo limekuwa kikwazo kwa watalii hao.

Serikali imepanga kuanzisha vituo vya kuwekea mafuta ya ndege mahali vilipo vivutio vya utalii ili kuziwezesha ndege ndogo kufika kwa urahisi na kupata huduma ya kuongeza mafuta hivyo kupunguza gharama kwa wasafiri wanaotembelea hifadhi za eneo hilo na ndege ambazo hulazimika kurudi jijini Dar es salaam kupata huduma hiyo. 
Aidha amesema katika mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali itanunua  ndege ndogo za abiria ili kuwezeha watalii kufika kwa urahisi katika maeneo ya hifadhi za Taifa.

UTAMBUZI WA MAENEO MAPYA YA UTALII.
Serikali kwa kushirikiana na Wakuu wa wilaya, mikoa na Wabunge itaanzisha mpango mpya kuviorodhesha vivutio vyote vya utalii vilivyo katika maeneo yao ili viweze kutangazwa ipasavyo na kuongeza kuwa mara baada ya kukamilika kwa mpango huo itaandaliwa orodha ya vivutio hivyo ili vianzwe kutangazwa rasmi.
Katika kuimarisha shughuli za utalii nchini serikali itaweka mkazo katika uimarishaji wa utalii wa utamaduni, uimarishaji wa maeneo ya historia na Malikale ili kuwezesha eneo hilo kuchangia zaidi katika Pato la Taifa.

ULINZI NA USALAMA WA HIFADHI ZA TAIFA.
Prof. Maghembe ameeleza kuwa suala la ulinzi na usalama wa hifadhi zote za Taifa liko kwa mujibu wa sheria na kubainisha kuwa serikali imeanzisha Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania(TAWA) litakalochukua mbuga zote zilizokuwa na uongozi ambazo ziko nje ya TANAPA.
Jeshi hilo litapambana kikamilifu na ujangili, kuimarisha maadili na nidhamu ya askari wa ulinzi wa hifadhi za taifa pamoja na kushughulikia maslahi yao na kuondoa migogoro kati ya askari na wananchi.
Amesisitiza kuwa mara baada ya Bunge la Bajeti, Wizara itakutana na wahifadhi wakuu wote ili kuweka vigezo vya kuzingatia katika majukumu yao na kusisitiza kuwa wahifadhi wote watakaoshindwa kwenda na kasi ya vigezo vilivyowekwa hawatajumuishwa kwenye jeshi hilo.

Aidha, amekemea vikali vitendo vinavyofanywa na baadhi ya askari wa hifadhi kupiga raia na kuchoma nyumba za wananchi kuwa havikubaliki na ni kinyume cha majukumu yao.
"Nimesikiliza kwa makini michango ya wabunge na nimesikia wafanyakazi katika hifadhi zetu wanapiga raia wanaua mifugo na kuchoma nyumba za wananchi jambo ambalo halikubaliki, hatukuwatuma kufanya hivyo" Amesisitiza Prof.Maghembe.
KUSHUGHULIKIA MIGOGORO YA MIPAKA MAENEO YA HIFADHI.
Serikali imesema mpaka sasa kuna migogoro ya ardhi 281, kati ya hiyo 35 ambayo ni sawa na asilimia 12.5 ni migogoro ya hifadhi na kuita  Mikoa yenye migogoro hiyo kuwa ni pamoja na Mara , Tanga na Kagera inachukua jumla ya asilimia 50.
Aidha, amesema kuwa mkoa wa Tabora unaongoza kwa kuwa na eneo kubwa la ardhi na unaongoza kwa kuwa na migogoro mingi ya hifadhi kwa asilimia 40.
Katika kuishughulikia migogoro hiyo Serikali imeziagiza wizara za Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Maji na Umwagiliaji, TAMISEMI, Nishati na Madini, Ofisi ya Makamu wa Rais - Mazingira pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii kushirikiana pamoja katika kutatua migogoro yote ya ardhi nchini.

 UBORESHAJI WA MAENEO YA HIFADHI NA MAMLAKA ZA UHIFADHI.
Amesema katika mwaka wa fedha wa 2016/2017 kiasi cha shilingi bilioni 1 kimetengwa kushughulikia usafi wa mazingira na ujenzi wa vyoo vya kisasa  katika hifadhi ya mlima Kilimanjaro vitakavyokuwa na uwezo wa kugeuza maji taka kuwa poda kwenye njia zote za kupandia kwenye mlima huo ili kuweka mazingira ya mlima huo kuwa safi.
Aidha,amesema kuwa Mamlaka za hifadhi za Taifa zimeendelea kuchangia katika maendeleo ya wananchi katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo ujenzi wa madarasa, miundombinu ya barabara, utoaji wa madawati katika halmashauri mbalimbali nchini.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa