MBUNGE wa Ulanga, Godluck Mlinga (CCM) ameyatuhumu mashirika ya umma
ambayo hayajajiunga na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kuwa
watendaji wake wakuu wamepewa malipo ya asilimia 10 ili mashirika hayo
kujiunga na kampuni binafsi za bima.
Ameyataja baadhi ya mashirika hayo ya umma yaliyokaidi kujiunga na
NHIF licha ya kulazimishwa kisheria kuwa ni Mamlaka ya Udhibiti wa
Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Mamlaka ya Udhibiti wa Mawasiliano
Tanzania (TCRA) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
“Yapo mashirika ya umma yanakataa kujiunga na NHIF wakati sisi
wabunge tumejiunga, wao ni nani? Wakubwa wao wanapata asilimia 10 na
wanajiunga na kampuni za bima ya afya binafsi…
“Mimi niliwahi kuwa Compliance Officer wa NHIF nikaenda TRA,
nikawaeleza umuhimu wa kujiunga NHIF unachangia pesa kidogo unapata
huduma nyingi lakini bosi wao akanijibu pesa si tatizo na afadhali
ametumbuliwa huyo bosi wao, yule angekuwa ofisini kwangu asingetoka,”
alisema Mlinga na kuongeza:
“Kila sehemu wananitaja Mlinga Mlinga, napata vitisho vingi lakini
serikali inanilinda na kama jeshi (JWTZ) limeweza kusambaratisha M23
itashindwa kunilinda mimi…wengine wananiita teja hivi teja anavaa suti
iliyonyooka kama mimi, siwezi kukasirika kwa sababu si kweli lakini
wangeniita mbilikimo ningekasirika kwa sababu kweli.”
Mbunge huyo alitaka serikali ikomeshe tabia ya wanaume kubaka wazee
na kufafanua “najiuliza wanawake wa mikoa yenye ubakaji wa wazee ni
wagumu kuelewa hadi wazee wabakwe?”
Naye Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabiby (CCM) amesema sasa ataanza kuacha
kuwashawishi wananchi wake kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF)
kutokana na mfuko huo kutopeleka dawa na chanjo za watoto kwenye vituo
vya afya, badala yake inapeleka kondomu na vifaa visivyo muhimu kwa
wananchi.
0 comments:
Post a Comment