WIZARA ya Maliasili na Utalii imetangaza kufanya sensa ya mamba na viboko nchi nzima.
Waziri Profesa Jumanne Maghembe alisema hivi karibuni kwamba, kazi
hiyo itafanywa na Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI).
Katika hotuba yake ya bajeti ya wizara hiyo bungeni mjini hapa,
Maghembe alisema taasisi hiyo itafanya sensa ya wanyamapori katika
sehemu mbalimbali za ndani na nje ya nchi ya maeneo yaliyohifadhiwa.
“Maeneo hayo ni pamoja na mfumo wa ikolojia ya Serengeti. Aidha,
taasisi itafanya sensa ya mamba na viboko nchi nzima,” alisema Maghembe.
Alisema itaendelea na majaribio ya matumizi ya ndege zisizo na rubani
katika kuzuia tembo waharibifu wa mazao katika mifumo ikolojia ya
Tarangire-Manyara na Serengeti kupunguza mgongano kati ya tembo na
binadamu.
Aliongeza pia kuwa Tawiri imekamilisha utafiti kuhusu ugonjwa wa Homa
ya Bonde la Ufa (RVF) ambao umekuwa ukitokea nchini kila baada ya miaka
10 hadi 15.
Alisema utafiti huo umeonesha kuwa kirusi cha ugonjwa wa RVF
kinatunzwa kwa kiwango cha chini kwenye mbu jamii ya Aedes na Culex –
asilimia 2.7, wanyama wafugwao ng’ombe asilimia 5.7, kondoo na mbuzi 1.9
na wanyamapori wastani wa asilimia 14.6.
Chanzo Kutoka Habari Leo
0 comments:
Post a Comment