Na Benedict Liwenga, MAELEZO, Dodoma.
SERIKALI
za Vijiji nchini zimekumbushwa kusimamia vizuri Sheria ya Ardhi Na. 5
ya mwaka 1999 ambayo imeweka utaratibu wa kufuata kwa mtu anayehitaji
kupata ardhi kwa matumizi mbalimbali.
Agizo
hilo limetolewa leo Bungeni Dodoma na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais,
Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mhe. Selemani Jafo wakati akijibu
swali la Mbunge wa Jimbo la Chemba, Mhe. Juma Nkamia ambaye alitaka
kujua utayari wa Serikali wa kufuta uamuzi uliotolewa na Mkuu wa Mkoa wa
Manyara wa kuwazuia wakulima ili kuondoa mgogoro wa muda mrefu.
Mhe.
Jafo ameeleza kuwa, tamko lililotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Manyara
liliwahusu wakulima waliokuwa wavamizi katika eneo la hifadhi ya
Wanyamapori ya Makame kutoka katika Wilaya za Kiteto, Babati, Chemba,
Kondoa na Mkoa wa Iringa waliokuwa wanaendesha shughuli za kilimoi
katioka hifadhi hiyo kinyume cha Sheria.
Amefafanua
kuwa, uamuzi huo ulitolewa kufuatia azimio la kikao cha pamoja cha
Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya za Kiteto cha Chemba kilichokaa
tarehe 12 Novemba, 2015.
“Kikao
hicho kilishirikisha viongozi wa Vijiji vitano vinavyounda Mamlaka ya
Hifadhi (WMA) ambavyo ni Ngobolo, Katikati, Ndedo, Irkiushbor na Makame
pamoja na wawakilishi wa wakulima 10 kutoka kila Wilaya”, alisema Mhe.
Jafo.
Aidha,
kwa mujibu wa Sheria, hairuhusu shughuli yoyote ya kibinadamu ikiwemo
kilimo, ufugaji au makazi kuendeshwa katika hifadhi.
“Naomba
kutoa wito kwa wananchi kuzingatia Sheria za nchi ili kuepuka migogoro
katika jamii, Serikali za vijiji zinakumbushwa kusimamia vizuri Sheria
ya Ardhi Na. 5 ya mwaka 1999 ambayo imeweka utaratibu wa kufuata kwa mtu
anayehitaji kupata ardhi kwa matumizi mbalimbali, lengo ni kuzuia
migogoro ya ardhi isiyokuwa ya lazima ambayo kwa sehemu kubwa inatokana
na kutozingatiwa kwa Sheria za ardhi”, alisema Mhe. Jafo.
0 comments:
Post a Comment