Home » » SHERIA MPYA YA USHIRIKA YAWANUFAISHA WAKULIMA WA TUMBAKU

SHERIA MPYA YA USHIRIKA YAWANUFAISHA WAKULIMA WA TUMBAKU



Na Fatma Salum- MAELEZO, Dodoma.

Serikali imebainisha kuwa Sheria Mpya ya Ushirika (Sheria namba 6 ya mwaka 2013) imesaidia kupunguza changamoto za wanachama wa Vyama vya Ushirika pamoja na wakulima wa Tumbaku nchini.

Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi  Mhe. Tate William Ole-Nasha aliyasema hayo leo bungeni Mjini Dodoma wakati akijibu maswali ya wabunge kwenye kipindi cha maswali na majibu.
 
Mhe. Ole-Nasha alisema kuwa baadhi ya marekebisho ya Sheria hiyo yanayowanufaisha wanachama wa Vyama vya Ushirika wakiwemo wakulima wa tumbaku ni pamoja na kuwachukulia hatua viongozi wabadhirifu wa vyama hivyo.

“ Katika maeneo yanayolima tumbaku viongozi wabadhirifu wa Vyama vya Ushirika 26 Mkoani Ruvuma  wakiwemo Maafisa Ushirika wawili wamesimamishwa kazi na kufikishwa mahakamani.” alisema Ole-Nasha.
Pia Mhe. Ole-Nasha alifafanua kuwa sheria ya sasa inakataza vyama kukopa zaidi ya asilimia 30 ya mali zake (Own Capital) ili kuzuia vyama hivyo kuingia kwenye madeni makubwa yasiyolipika  na hatimaye kusababisha migogoro ndani ya vyama.

Akizungumzia mafanikio upande wa tozo, Ole-Nasha lisema kuwa kuanzia sasa Mkutano Mkuu utakuwa chini ya uenyekiti huru utakaochaguliwa na wajumbe wa mkutano huo kinyume na awali ambapo Mwenyekiti wa Bodi ya Tumbaku ndiye aliyekuwa Mwenyekiti wa Mkutano Mkuu. 


“Lengo ni kulinda maslahi ya wakulima ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa tozo zote zinazoidhinishwa na Mkutano Mkuu zinakuwa na maslahi kwa wakulima wa Tumbaku.” Aliongeza Ole-Nasha.

Kwa mujibu wa Ole-Nasha Serikali inatambua uwepo wa kodi nyingi na tozo kwenye mazao mbalimbali ya chakula na biashara hivyo kwa kushirikiana na wadau imedhamiria kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara katika sekta ya kilimo kwa kupitia upya taratibu, vibali, tozo, kodi, ushuru na ada nyingine zinazotozwa ili kutoa nafuu kwa wakulima.    

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa