Home » » ‘Ma-RC msiomaliza madawati kaeni chonjo’

‘Ma-RC msiomaliza madawati kaeni chonjo’

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo amewanyooshea kidole wakuu wa mikoa nchini wanaosuasua katika agizo la rais la kuhakikisha kila shule ya msingi na sekondari, inakuwa na madawati ifikapo mwisho wa mwezi huu.
Alisema hayo jana wakati akifungua majengo mapya matatu ya Shule ya Msingi Nzuguni B katika Manispaa ya Dodoma, ambayo yamejengwa kwa nguvu za wananchi na wadau. Jaffo alisema katika maeneo mengi, kazi ya utengenezaji madawati inakwenda vizuri kwani katika mikoa mingi hali inaonesha kazi hiyo inakwenda vizuri.
“Wakuu wa mikoa wanaosuasua watapimwa kwa kigezo hicho katika utendaji kazi wao,” alisema Naibu Waziri. Alisema baada ya Juni 30, ambayo ndiyo siku iliyowekwa katika kuhakikisha kila shule inakuwa na madawati, itafanyika tathimini nchi nzima kuona kama kazi hiyo imefanikiwa.
“Niwatie moyo wakuu wa mikoa kazi yao ni nzuri na waendelee kujipanga katika kuhakikisha wanatimiza kazi hii,” alisema na kuongeza kuwa Aprili alifanya ziara katika shule hiyo na kukuta ikiwa na changamoto nyingi ikiwemo uhaba wa vyumba vya madarasa huku wanafunzi wakiwa wamekaa chini kutokana na uhaba wa madawati.
Pia katika shule hiyo kulikuwa na vyumba vitatu vya madarasa ambavyo vilikuwa havijakamilika ndipo alipoagiza kukamilishwa kwa majengo hayo na wanafunzi kupatiwa madawati. Alisema agizo hilo limetekelezwa kikamilifu na majengo hayo yamekamilika huku madawati 264 kati ya 400 tayari yamepelekwa shuleni hapo na wanafunzi wanakalia.
Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Dodoma, Azimina Mbilinyi alisema changamoto kubwa iliyokuwepo katika shule hiyo ilikuwa uhaba wa madawati, ambayo awali kulikuwa na madawati 84 kati ya 568 yaliyohitajika.
Mbunge wa Dodoma Mjini, Antony Mavunde alisema ataendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo. Mavunde ambaye pia ni Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Ajira, Kazi na Vijana alitoa Sh 300,000 ili huduma ya maji irudishwe huku akiahidi kusaidia kompyuta.
Chanzo Gazeti La Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa