Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma
Naibu
Spika Mhe. Dkt. Tulia Ackson ameshiriki harambee ya kuchangia waandishi
wa habari kwa ajili ya kuwakatia Bima ya Afya “Media Car Wash For
Health” iliyofanyika leo katika viwanja vya Jamhuri Mjini Dodoma ambapo
amechangia jumla ya shilingi milioni 5 ili kuokoa maisha ya waandishi wa
habari.
“Kuna
umuhimu mkubwa wa kuwachangia waandishi wa habari kwani wamekuwa na
mchango mkubwa katika kuleta maendeleo ya nchi na kuhamasisha amani ya
nchi, kwa kutambua umuhimu wao nitachangia shilingi 5,000,000 ili iweze
kuwakatia Bima ya Afya,” alisema Mhe.Dkt. Tulia.
Licha
ya kuchangia fedha hizo Mhe. Tulia aliosha baadhi ya magari ya
waheshimiwa wabunge kwa ajili ya kuchangia harambee hiyo ambapo kila
mbunge aliyeoshewa gari yake alichangia shilingi 100,000 ambazo moja kwa
moja ziliingia katika mfuko wa kuokoa maisha ya waandishi wa habari kwa
kuwakatia Bima ya Afya.
Kwa
upande wake, Naibu Waziri wa Afya, Maendelea ya Jamii, Jinsia, Wazee na
Watoto Mhe. Hamis Kigwangalla amechangia shilingi 1,000,000/= ambayo
nayo inaenda kusaidia waandishi wa habari ili waweze kukatiwa Bima ya
Afya.
Lengo la harambee hiyo ni kukusanya zaidi ya shilingi milioni 200 ambazo zitatumika kuwakatia Bima ya afya zaidi ya waandishi wa habari 1000 hapa nchini. Aidha
harambee hii ni ya pili, harambee nyingine kama hii ilifanyika mwaka
2015, viwanja vya Leaders jijini Dar es Salaam na kufanikiwa kukusanya
shilingi milioni 30 ambazo zilisaidia kugharamia matibabu kwa waandishi
watatu waliokuwa wanaugua kwa kipindi kirefu.
0 comments:
Post a Comment