Jonas Kamaleki
Maelezo
Dodoma
Serikali imekubaliana na mifuko ya hifadhi ya jamii kuanza utekelezaji wa ujenzi wa viwanda nchini ili kuhakikisha kuwa adhma ya Tanzania ya kufikia uchumi wa viwanda inafanikiwa ifikapo mwaka 2020.
Hatua hiyo ni utekelezaji wa agizo la Rais John Pombe Magufuli aliyeitaka mifuko hiyo kuwekeza katika ujenzi wa viwanda nchini.
Akizungumza
mara baada ya kikao cha pamoja baina ya Serikali na mifuko hiyo, Waziri
wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira, na
Ulemavu, Jenister Mhagama alisema Serikali imekusudia kuhakikisha
uanzishwaji wa viwanda unaanza haraka na kuongeza fursa za ajira nchini.
Mhagama
alisema kuwa mali ghafi na nguvu kazi ya kutosha zipo hapa nchini hivyo
hakuna sababu ya kuchelewa kuanza, ambapo Serikali imepanga hadi
kufikia mwishoni mwa mwaka 2016, utekelezaji wa adhma hiyo inaanza
kuonekana machoni mwa Watanzania.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa sekta ya hifadhi ya Jamii (SSRA)alisema, Irene Isaka alisema ni
agizo hilo limekuja katika wakati mwafaka kwa kuzingatia kuwa kwa
mifuko ya Hifadhi ya jamii imekusudia kutekeleza kwa vitendo adhma ya
Serikali ya awamu ya tano inayosisitiza kuijenga Tanzania kupitia uchumi
wa viwanda.
Kwa
mujibu wa Isaka alisema kuwa kanuni na mifumo ya mifuko hiyo inaruhusu
suala la uwekezaji katika viwanda ama kwa njia ya ubia au ya hati
fungani au kutoa mikopo kwa wanotaka kuwekeza katika viwanda.
Naye
Katibu Mkuu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Dkt, Adelhelm
Meru alisema uwekezaji katika viwanda ni suala ambalo linawashirikisha
wadau wengi zikiwemo wizara za Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa ajili ya
malighafi za viwandani, Elimu kwa ajili ya ujuzi wa watu wa kufanya kazi
viwandani na Wizara ya Nishati na Madini kwa ajili ya nishati ya
kuendesha viwanda.
“Kwa
kuangalia raslimali tulizo nazo tumewaomba wadau waanze na viwanda
ambavyo vilikuwepo lakini kwa sasa havifanyi kazi kama vile Shirika la
Usagishaji la Taifa (NMC), General Tyre, NARCO na Kiwanda cha Viwadudu
cha Kibaha, alisema Dr. Meru na kuongeza kuwa malighafi za viwanda hivi zinapatikana hapa nchini.
0 comments:
Post a Comment