Home » » Serikali yawataka wanamichezo kujiepusha na matumizi ya dawa za kuongeza nguvu mwilini au matumizi ya dawa zisiruhusiwa kwa wanamichezo

Serikali yawataka wanamichezo kujiepusha na matumizi ya dawa za kuongeza nguvu mwilini au matumizi ya dawa zisiruhusiwa kwa wanamichezo

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Na Anna Nkinda - Dodoma
 Serikali imewataka wanamichezo kujiepusha na matumizi ya dawa za kuongeza nguvu mwilini au matumizi ya dawa zisiruhusiwa kwa wanamichezo kwa kufanya hivyo wanaweza kupata madhara ya kiafya na  kufungiwa kushiriki katika mashindano ya kitaifa na kimataifa.

Mwito huo umetolewa leo na Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Anastazia Wambura wakati akifunga mashindano ya michezo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu vilivyopo mkoani Dodoma yaliyofanyika katika uwanja wa Jamhuri uliopo mkoani humo.

Mashindano hayo yaliyojumusha wanafunzi kutoa vyuo vikuu vya Dodoma, Mipango, St. John na Chuo cha Biashara (CBE) yaliandaliwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa Pensheni wa PSPF .

Mhe. Wambura alisema kwa kipindi cha mwaka 2015/16 wanamichezo 14 walichukuliwa vipimo vyao na kupelekwa katika maabara za Kimataifa na wote kukutwa salama na hivyo kuwapongeza  wanamichezo hao ambao wameweza kujilinda kwa kutotumia dawa hizo.

Alisema, “Viongozi wote wa Vyama vya Michezo, waalimu na madaktari wa wanamichezo tuungane  kwa pamoja kupiga vita matumizi ya dawa za kuongeza nguvu michezoni.  Msisite kuchukua hatua kali pale inapothibitika bila shaka yeyote kuwa mwanamichezo ametumia dawa za kuongeza nguvu mwilini”.

Mhe. Naibu Waziri pia aliwasisitiza wanafunzi wa vyuo vyote nchini kushiriki katika michezo na kusoma kwa bidii ili waweze kujikwamua kiuchumi na kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa Taifa.

“Vijana wakitumia muda wao wa ziada kushiriki katika Michezo watajiepusha na mazingira hatarishi  yatakayowapelekea kuwa wazurulaji, kupata maambukizi ya VVU, kutumia dawa za kulevya na kushiriki katika vitendo vya uhalifu”, alisisitiza Mhe. Wambura.

Aidha Mhe. Naibu Waziri huyo aliwakumbusha Wajumbe wa Bodi ya Wadhamini wa PSPF waendelee kudhamini michezo kama hiyo ili kuweza kuhamasisha vijana kushiriki katika michezo kwani Michezo ni ajira, afya na inaimarisha umoja.

Mhe. Naibu Waziri alisema, “Napenda kuwahakikishia mkifanya hayo hakika mtaendelea kuwa Mfuko wa chaguo la kwanza kwa wanachama wapya kama ilivyo hivi sasa, kwani hawa wanafunzi ndio wanachama wa baadae haswa ikizingatiwa hivi sasa kinachovutia wanachama wapya ni huduma bora na kuwajali wateja wenu”.

Kwa upande wake Afisa Mfawidhi wa PSPF wa  Mkoa wa Dodoma Salim Kimbute aliwaomba wanafunzi walioshiriki katika mashindano hayo kufikisha elimu kwa jamii hususani vijana ambao wameajiriwa au wanaotarajiwa kuajiriwa hivi karibuni katika maeneo mbalimbali ili nao waweze kufurahia maisha bora ya sasa na baadaye kwa kujiunga na PSPF.

“Katika kuhakikisha PSPF inakuwa karibu na jamii, Mfuko unafadhili mashindano kwa wanafunzi wa vyuo katika Mikoa mbalimbali ili kuweza kuwahamasisha kushiriki katika michezo na vilevile kuwapa elimu ya hifadhi ya jamii ili kuhakikisha kila Mtanzania anafaidika na Hifadhi ya Jamii”, alisema Kimbute.

PSPF iliandaa mashindano hayo ili kuweza kuhamasisha na kutoa fursa kwa wanafunzi kujifunza umuhimu wa michezo na hifadhi ya jamii.

Washindi wa kwanza katika mashindano hayo ambao walishiriki michezo ya mpira wa pete, miguu, wavu na kikapu walipewa zawadi ya Kombe na vifaa vya michezo, na washindi wengine walipewa zawadi za vifaa vya  michezo.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa