Na Benny Mwaipaja,
WFM
KATIBU Mkuu wa Wizara
ya Fedha na Mipango, Dkt. Servacius Likwelile amesema kuwa Tanzania imejipanga
kuimarisha mapato yake ya ndani ili kutekeleza kikamilifu Mpango wa Pili wa Taifa
wa Maendeleo wa mwaka 2016/2017 hadi 2020/2021.
Dkt. Likwelile,
amesema hayo Mjini Dodoma, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa siku 2
unaowahusisha wataalamu wa Uchumi na Mipango wapatao 170 kutoka nchi nzima.
Amesema kuwa misaada
kutoka kwa wadau wa maendeleo imekuwa ikipungua kila wakati, hatua ambayo
imeifanya Serikali kuendelea kujipanga kukabiliana na nakisi ya Bajeti yake ili
kukuza maendeleo.
"Mikopo yenye
riba nafuu nayo imepungua, sasa hivi unaenda kukopa kibiashara, kwa uchumi wetu
huu hatuwezi kumudu" alisisitiza Dkt. Likwelile
Ameeleza kuwa
Tanzania inakabiliwa na changamoto kubwa ya kuimarisha miundombinu ya barabara,
reli, bandari na mambo mengine, hali inayohitaji fedha nyingi ambazo zitapatika
kwa kukusanya kodi mbalimbali.
Amewataka wataalamu
hao wa uchumi na mipango kujadili na kuibuka na mipango itakayosaidia
kufanikisha utekelezaji wa Mpango huo wa Pili wa Maendeleo wa Taifa unaotarajiwa
kugharimu shilingi Trilioni 107.
Akifungua mkutano huo
kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, Waziri wa Katiba
na Sheria Dkt. Harrison Mwakyembe amewataka wataalamu hao kutoa mapendekezo ya
kitaalamu wakizingatia changamoto mbalimbali zikiwemo za kupanda kwa gharama za
mafuta duniani.
Vilevile,
amewakumbusha umuhimu wa kutumia takwimu sahihi wakati wa kupanga namna bora ya
kutekeleza mpango huo unaosubiriwa kwa hamu kubwa na watanazania kuwaletea
maendeleo ya haraka
"Takwimu ndizo
zinazotoa picha halisi ya matatizo yanayowakabili watanzania ukiwemo umasikini,
ambapo zikitumika vizuri zitasaidia kupanga namna bora ya wananchi wanavyoweza
kuondokana na umasikini huo" Alisisitiza Dkt. Mwakyembe
Kwa upande wake,
Kaimu Katibu Mtendaji wa Tume ya Mipango, Florence Mwanri, amesema kuwa
Tanzania imedhamiria kuwa nchi yenye uchumi wa kipato cha kati ifikapo mwaka
2025.
Amesema kuwa hatua
hiyo itafikiwa kwa kuelekeza nguvu kubwa katika uanzishwaji na uendelezaji wa
viwanda kwa kushirikiana na sekta binafsi.
Mwanri amesema kuwa
hatua hiyo itakuza uchumi wa nchi kwa kuongeza kipato cha wananchi pamoja na
ajira na akasisitiza umuhimu wa wananchi kufanya kazi kwa bidii na kujitolea
utaalamu na nguvu zao zote kufanikisha malengo hayo.
End
0 comments:
Post a Comment