KAMBI Rasmi ya Upinzani Bungeni imeweka msimamo wa kutohudhuria kikao
chochote cha Bunge la Jamhuri ya Muungano kitakachoongozwa na Naibu
Spika, Dk Tulia Ackson, kwa maelezo kuwa amekuwa akivunja demokrasia kwa
kuwafanyia ubabe na kuwapendelea wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Msimamo huo ulitolewa jana na Kiongozi wa Kambi hiyo, Freeman Mbowe
nje ya Ukumbi wa Msekwa ulio katika Viwanja vya Bunge, muda mfupi baada
ya wabunge wanaoiunda kambi hiyo kutoka nje ya Bunge walipoona kuwa
Naibu Spika ndiye aliyepaswa kuendesha kipindi cha maswali na majibu
asubuhi.
Kwa mujibu wa Mbowe, hawataona tabu kuendelea na utaratibu huo wa
kususia vikao vinavyoendeshwa na Dk Tulia hata kama itakuwa ni vipindi
vyote hadi Bunge livunjwe kwa sababu lengo lao ni kupinga uonevu na
ubabe anaowafanyia.
“Tunaenda nje ya maeneo haya ya Bunge kukutana na wabunge wenzetu
waliofukuzwa ili tujadili mambo ya msingi ambayo ni pamoja na kuweka
mkakati wa kuwazungukia wananchi kuwaeleza juu ya uonevu wa Naibu Spika
wachukue hatua kwa sababu ndio waliotuchagua.
Tunaenda kumshtaki Dk Tulia kwa wananchi,” alisema. Alieleza kuwa,
hawako tayari kuona Naibu Spika akiunga mkono kusimamishwa kwa wabunge
muhimu wa kambi hiyo, hivyo kuendeleza mgomo huo hata kama utakuwa
ukiwagharimu.
Alifafanua kuwa pindi atakapoongoza Bunge mtu mwingine watakuwa
wakihudhuria kwa sababu wao hawajalisusia Bunge wala mtu mwingine
isipokuwa Dk Tulia. Alisema makosa wanayodaiwa kuyafanya na kuadhibiwa
yanafanywa na wabunge wa Chama Cha Mapinduzi pia lakini wanashangaa
wanaobanwa ni wao pekee.
Chanzo Gazeti La Habari Leo
0 comments:
Post a Comment