Na: Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma
Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi katika kipindi
cha mwaka wa fedha 2016/2017 itabaini taasisi zote na watu binafsi
wanaodaiwa fidia na wananchi ili waweze kulipa fidia hizo.
Akiongea
leo Bungeni, mjini Dodoma Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Angelina
Mabula amesema kuwa ni kweli tatizo hilo lipo na tayari Serikali
imechukua hatua kwa kuzielekeza Halmashauri zote na taasisi nyingine
kulipa fidia stahiki kwa wananchi pale wanapotaka kutwaa maeneo yao.
Mhe.
Mabula amesema kuwa taasisi nyingi zimekuwa zikichukua mashamba ya
wananchi na kushindwa kuwalipa fidia hivyo kulimbikiza madeni hayo kwa
muda mrefu hali inayokwamisha shughuli za maendeleo.
“Halmashauri
za Wilaya, Taasisi na Maafisa Ardhi hawaruhusiwi kuchukua mashamba ya
wananchi kabla hawajakamilisha utaratibu wa malipo ya fidia kwa wananchi
hao, ili kuondokana na malimbikizo ya madeni ya fidia ambayo malipo
yake huchukua muda mrefu na kurudisha nyuma maendeleo ya wananchi,”
alisema Mhe. Mabula.
Aidha
Mhe. Mabula amewataka wananchi wanaodai fidia kuwa wavumilivu wakati
Wizara yake inaendelea kufanya upembuzi wa taasisi hizo ili ziweze
kulipa fidia zote zinazodaiwa na wananchi.
Vilevile
Wizara hiyo imetoa ramani za mitaa kwa wenyeviti wa mitaa wa Jiji la
Dar es Salaam ili wenyeviti hao waweze kutambua matumizi ya maeneo yao,
kwa mfano maeneo ya wazi, na nini kijengwe katika maeneo yao kama vile
nyumba fupi au ndefu, hoteli au chuo ili kuondokana na migogoro ya
kubolewa nyumba kwa kujenga eneo lisiloruhusiwa.
“Tumeanza
kwa mkoa wa Dar es Salaam lakini zoezi litaendelea kila Mkoa na kila
Wilaya Nchi nzima, ili Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji waweze kutambua
matumizi ya maeneo yao, hivyo kuchukua hatua kwa haraka pindi ambapo
maeneo hayo yanatumika tofauti na matumizi yaliyoko” alifafanua Mhe.
Mabula.
Aidha
Mhe. Mabula amezitaka Halmashauri kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi,
Nyumba, na Maendeleo ya Makazi kuwapa uwezo wenyeviti hao ili waweze
kufanya kazi hiyo kiufanisi.
0 comments:
Post a Comment