Home » » WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO KUSIMAMIA UKUAJI WA UCHUMI KWA MAENDELEO YA NCHI

WIZARA YA FEDHA NA MIPANGO KUSIMAMIA UKUAJI WA UCHUMI KWA MAENDELEO YA NCHI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 





Na Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma

WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameliambia Bunge Mjini Dodoma, Leo, Juni Mosi, 2016 kwamba serikali imejipanga kuchukua hatua madhubuti zinazolenga kujenga Taifa linalojitegemea kwa kukuza uchumi na kupunguza umasikini. 

Amezitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na  kusimamia na kufuatilia kwa ukamilifu utekekelezaji wa Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/17 - 2020/21. Mpango huu unajikita katika kujenga msingi wa uchumi wa viwanda na maendeleo ya watu.

Amesema kuwa ili mpango huu uweze kutekelezwa kwa ufanisi na kupata matokeo tarajiwa, ni dhahiri kuwa zinahitajika rasilimali za kutosha, hususan rasilimali fedha. 

"Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na wadau wengine inalo jukumu la kuimarisha ukusanyaji wa mapato ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa rasilimali fedha" alisisitiza

Dkt. Mpango amesema kuwa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015-2020 imeweka bayana majukumu ya Wizara ya Fedha na Mipango ya kuimarisha usimamizi na ukusanyaji wa mapato, kupanua wigo wa vyanzo vipya vya mapato na kusimamia kwa ufanisi matumizi ya fedha za umma kwa kuzingatia sheria, kanuni na miongozo mbalimbali.

Amenukuu kauli iliyotolewa na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa, alipokuwa anawasilisha hotuba yake katika Bunge, Aprili 25 mwaka 2016, aliposema kuwa  mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano yenye falsafa ya HAPA KAZI TU, imelenga kufikia kipato cha kati na kufanyika mapinduzi makubwa ya viwanda yanayotegemea sana utulivu wa uchumi.

"Tutasimamia kikamilifu matumizi ya vifaa na mifumo ya kielektroniki katika ukusanyaji wa mapato ili kuongeza ufanisi na kudhibiti upotevu wa mapato" Aliongeza Dkt. Mpango
Amesema kuwa serikali itarasimisha sekta isiyo rasmi kuingia katika mfumo wa kodi na hivyo kupanua wigo wa kodi na Kuimarisha ufuatiliaji wa mapato yanayokusanywa na taasisi na mamlaka mbalimbali za Serikali ili kuongeza ukusanyaji wa mapato ya Serikali.

Dkt. Mpango amebainisha kuwa watasimamia na kuimarisha ukusanyaji wa mapato yasiyo ya kodi na kuboresha usimamizi wake chini ya Mamlaka ya Mapato Tanzania kutokana na uzoefu na mifumo ya ukusanyaji iliyopo nchi nzima

"Tutaendelea kuchukua hatua za kudhibiti na kupunguza misamaha ya kodi isiyo na tija na Kuendelea kuimarisha usimamizi na kufanya ukaguzi wa mara kwa mara bandarini na maeneo ya mipakani ili kuhakikisha kwamba kodi stahiki zinakusanywa" aliongeza Dkt. Mpango.

Ametaja mikakati hiyo kuwa ni moja ya njia ya kupunguza utegemezi wa misaada kutoka nje ambayo imezidi kupungua kila mwaka.

Ametoa mfano wa mwaka wa fedha unaoishia Juni mwaka huu ambapo hadi Machi, wadau wa maendeleo wametoa shilingi bilioni 1,064.89 sawa na asilimia 46 ya fedha zote zilizoahidiwa kutolewa na wadau hao hali iliyoathiri utekelezaji wa miradi mbalimbali iliyokusudiwa

Ametaja sababu za hali hiyo kuwa ni kupungua kwa misaada toka nje kunatokana na kujiondoa kwa baadhi ya Washirika wa Maendeleo wanaochangia kupitia Misaada na mikopo ya kibajeti na baadhi ya Washirika wa Maendeleo kupunguza ahadi zao.

"Wafadhili wanaochangia kupitia misaada ya kibajeti walipunguza michango yao kutoka shilingi bilioni 660 mpaka shilingi bilioni 399 katikati ya mwaka wa fedha 2015/16 na wengine kuhusisha utoaji wa fedha na masharti ambayo hayakuwemo katika makubaliano ya awali" Aliongeza Dkt. Mpango

Alisema kuwa katika kushughulikia changamoto hizo, Serikali inaendelea na mazungumzo na Washirika wa Maendeleo ili kuhakikisha kwamba fedha zilizoahidiwa zinatolewa kwa wakati.
WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameliomba Bunge, liidhinishie Wizara yake kupitia mafungu yote tisa ya kibajeti, jumla ya Shilingi Trilioni 8.7 kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na shilingi Bilioni 791.99 kwaajili ya miradi ya maendeleo.

Amesema kuwa  Kati ya fedha hizo,shilingi bilioni 45.45 ni kwa ajili ya Mishahara na shilingi bilioni 8,671.04 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo.
 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa