Na Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma
WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango,
ameliambia Bunge Mjini Dodoma, Leo, Juni Mosi, 2016 kwamba serikali imejipanga kuchukua hatua madhubuti zinazolenga
kujenga Taifa linalojitegemea kwa kukuza uchumi na kupunguza umasikini.
Amezitaja hatua hizo kuwa ni pamoja na
kusimamia na kufuatilia kwa ukamilifu utekekelezaji wa Mpango wa Pili wa
Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/17 - 2020/21. Mpango huu unajikita katika
kujenga msingi wa uchumi wa viwanda na maendeleo ya watu.
Amesema kuwa ili mpango huu uweze kutekelezwa kwa ufanisi na kupata
matokeo tarajiwa, ni dhahiri kuwa zinahitajika rasilimali za kutosha, hususan
rasilimali fedha.
"Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na wadau wengine
inalo jukumu la kuimarisha ukusanyaji wa mapato ili kukabiliana na changamoto
ya upungufu wa rasilimali fedha" alisisitiza
Dkt. Mpango amesema kuwa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya
mwaka 2015-2020 imeweka bayana majukumu ya Wizara ya Fedha na Mipango ya
kuimarisha usimamizi na ukusanyaji wa mapato, kupanua wigo wa vyanzo vipya vya
mapato na kusimamia kwa ufanisi matumizi ya fedha za umma kwa kuzingatia
sheria, kanuni na miongozo mbalimbali.
Amenukuu kauli iliyotolewa na Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa,
alipokuwa anawasilisha hotuba yake katika Bunge, Aprili 25 mwaka 2016,
aliposema kuwa mwelekeo wa Serikali ya
Awamu ya Tano yenye falsafa ya HAPA KAZI TU, imelenga kufikia kipato cha kati
na kufanyika mapinduzi makubwa ya viwanda yanayotegemea sana utulivu wa uchumi.
"Tutasimamia kikamilifu matumizi ya vifaa na mifumo ya
kielektroniki katika ukusanyaji wa mapato ili kuongeza ufanisi na kudhibiti
upotevu wa mapato" Aliongeza Dkt. Mpango
Amesema kuwa serikali itarasimisha sekta isiyo rasmi kuingia katika
mfumo wa kodi na hivyo kupanua wigo wa kodi na Kuimarisha ufuatiliaji wa mapato
yanayokusanywa na taasisi na mamlaka mbalimbali za Serikali ili kuongeza ukusanyaji
wa mapato ya Serikali.
Dkt. Mpango amebainisha kuwa watasimamia na kuimarisha ukusanyaji wa
mapato yasiyo ya kodi na kuboresha usimamizi wake chini ya Mamlaka ya Mapato
Tanzania kutokana na uzoefu na mifumo ya ukusanyaji iliyopo nchi nzima
"Tutaendelea kuchukua hatua za kudhibiti na kupunguza misamaha ya
kodi isiyo na tija na Kuendelea kuimarisha usimamizi na kufanya ukaguzi wa mara
kwa mara bandarini na maeneo ya mipakani ili kuhakikisha kwamba kodi stahiki
zinakusanywa" aliongeza Dkt. Mpango.
Ametaja mikakati hiyo kuwa ni moja ya njia ya kupunguza utegemezi wa
misaada kutoka nje ambayo imezidi kupungua kila mwaka.
Ametoa mfano wa mwaka wa fedha unaoishia Juni mwaka huu ambapo hadi
Machi, wadau wa maendeleo wametoa shilingi bilioni 1,064.89 sawa na asilimia 46 ya fedha zote zilizoahidiwa
kutolewa na wadau hao hali iliyoathiri utekelezaji wa miradi mbalimbali
iliyokusudiwa
Ametaja sababu za hali hiyo kuwa ni kupungua kwa
misaada toka nje kunatokana na kujiondoa kwa baadhi ya Washirika wa Maendeleo
wanaochangia kupitia Misaada na mikopo ya kibajeti na baadhi ya Washirika wa
Maendeleo kupunguza ahadi zao.
"Wafadhili wanaochangia kupitia misaada ya
kibajeti walipunguza michango yao kutoka shilingi
bilioni 660 mpaka shilingi bilioni
399 katikati ya mwaka wa fedha 2015/16 na wengine kuhusisha utoaji wa fedha
na masharti ambayo hayakuwemo katika makubaliano ya awali" Aliongeza Dkt.
Mpango
Alisema kuwa katika kushughulikia changamoto hizo,
Serikali inaendelea na mazungumzo na Washirika wa Maendeleo ili kuhakikisha
kwamba fedha zilizoahidiwa zinatolewa kwa wakati.
WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango,
ameliomba Bunge, liidhinishie Wizara yake kupitia mafungu yote tisa ya
kibajeti, jumla ya Shilingi Trilioni 8.7 kwa ajili ya Matumizi ya
Kawaida na shilingi Bilioni 791.99 kwaajili
ya miradi ya maendeleo.
Amesema kuwa
Kati ya fedha hizo,shilingi bilioni
45.45 ni kwa ajili ya Mishahara na shilingi bilioni 8,671.04 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo.
0 comments:
Post a Comment