Na: Lilian Lundo – Dodoma – Maelezo
Wizara ya Fedha na Mipango leo Mjini Dodoma imetoa semina Kuhusu ubia kati ya Sekta Umma na Sekta Binafsi kwa wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Semina hiyo iliyofunguliwa na Naibu Spika Mhe. Tulia Ackson ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye semina hiyo ambapo mada kuhusu utaratibu huo iliwasilishwa na Kamishna anasimaia Idara inayoratibu ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi kutoka Wizara hiyo Dkt. Frank Mhilu.
“Ubia
kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi ni mkataba wa muda mrefu wa
kuanzia miaka 5 hadi 30 na kuendelea kati ya kampuni ya mwekezaji
binafsi na Taasisi ya Serikali ambapo mwekezaji binafsi anajenga
miundombinu au anapewa miundombinu ili aiboreshe kwa lengo la kutoa huduma ya umma kwa gharama nafuu na baada ya mkataba kwisha miundombinu husika hurejeshwa kwa Serikali,” alifafanua Dkt. Mhilu.
Aidha Dkt. Mhilu aliendelea kusema
kuwa, ili kufanikiwa katika ubia lazima kuwe na maandalizi muhimu
ambayo ni kuibua fursa za uwekezaji kwa mujibu wa mpango wa Taifa wa
maendeleo, kufanya uchambuzi yakinifu ili kujiridhisha kuwa mradi una
manufaa kwa uwekezaji kwa utaratibu wa ubia.
Vile
vile kuandaa ardhi na miundombinu wezeshi, kutangaza miradi kwa uwazi,
kujiridhisha ubora wa zabuni ya mwekezaji na namna ambavyo fedha
zitapatikana na uwezo wa Taasisi ya Umma kusimamia mradi husika.
Pia
Dkt. Mhilu aliitaja miradi ambayo iko katika hatua mbalimbali za ubia
kuwa ni mradi wa mabasi ya haraka Dar es Salaam (DART), mradi wa kufua
umeme wa Kinyerezi III (TANESCO), mradi wa barabara ya tozo wa Dar
– chalinze (TANROADS), mradi wa uzalishaji wa madawa muhimu (MSD) pia
iko miradi ambayo imechambuliwa na kutolewa taarifa zake kwa ajili ya
kuboreshwa.
Dkt.
Mhilu amesema kuwa utaratibu wa ubia sasa utakuwa kwenye ofisi moja
ambayo ni Wizara ya Fedha na Mipango ili kuweka ufanisi katika
utekelezaji wake ikiwa ni maamuzi ambayo yamefanyika katika awamu ya
Tano ya Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli.
Miradi
ya ubia ni mkombozi katika kuboresha Bajeti ya Serikali na kuharakisha
maendeleo endapo tu fursa za uwekezaji zitabuniwa vizuri, miradi
itaandaliwa vizuri na taarifa sahihi zitatumika katika kuandaa miradi,
wawekezaji wapatikane kwa njia ya haki, uwazi na
ushindani pamoja na mwekezaji kusimamiwa vyema katika ujenzi, uendeshaji
na urejeshaji wa miundombinu.
0 comments:
Post a Comment