HUZUNI imetanda katika wilaya ya Kongwa mkoani Dodoma, baada ya ajali
ya moto wa kibatari kuteketeza watoto wanne wa mama mmoja, waliokuwa
wamefungiwa chumbani na dada anayewalea.
Ajali hiyo ilitokea usiku wa kuamkia jana katika mtaa wa Nyerere, mji
mdogo wa Kibaigwa wilayani Kongwa, wakati mama wa watoto hao
aliposafiri kwenda shambani Kiteto mkoani Manyara, kwa ajili ya kuvuna
mazao na kuwaacha watoto wake mikononi mwa dada, aliyekuwa akimsaidia
kuwalea.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi mkoani
Dodoma, Lazaro Mambosasa alisema chanzo cha ajali hiyo ni mlipuko wa
kibatari kilichokuwa ndani ya chumba walicholala watoto hao, ambacho
kilichoma godoro na kuteketeza nyumba yote.
Moto huo ulioanzia katika chumba hicho, umeelezwa kuteketeza nyumba
yote ya vyumba sita iliyojengwa kwa tofali za udongo mali ya Nelson
Mdachi.
Kamanda Mambosasa aliwataja watoto hao kuwa ni Elizabeth Nelson (11)
mwanafunzi wa darasa la saba, Samweli Mdachi (7) anayesoma darasa la
kwanza na Nase Mgomba (9) anayesoma darasa la pili katika shule ya
msingi Miembeni na Peter Lema (9) mwanafunzi darasa la tatu shule ya
msingi St Paulo.
Kutokana na ajali hiyo, Kamanda Mambosasa amewakumbusha wazazi
wasiache watoto peke yao nyumbani kwa kuwa ni hatari kwani ajali
ikitokea ni vigumu kuokolewa.
Taarifa kutoka kwa watu wa karibu na majirani wa familia hiyo,
zimedai kuwa mama wa familia hiyo alikwenda shambani kuvuna mazao katika
wilaya ya Kiteto, mkoani Manyara na kuwaacha watoto hao chini ya
uangalizi wa msichana aliyefahamika kwa jina moja la Ester.
Kwa mujibu wa madai yao, ilipofika usiku Ester anayetajwa kuwa na
jukumu la kulea watoto hao, alitoka na kwenda kusikojulikana huku
akiwafungia watoto hao kwa nje.
Mkazi wa Kibaigwa, Denis Luhunga, alipozungumza na gazeti hili kuhusu
ajali hiyo alidai kuwa kibatari kilipolipuka, kilisababisha godoro
kushika moto na kuteketea kwa watoto hao. “Aliwafungia watoto ndani
akaacha kibatari kinawaka, baada ya kulipuka moshi mwingi ulijaa ndani,”
alidai Luhunga.
Kuhusu alipo baba wa familia hiyo, mkazi mwingine wa eneo la tukio
hilo, Paulo Sauli alisema baba wa watoto hao, aliyemtaja kwa jina la
Nelson Mdachi, alishakufa miaka mitatu iliyopita na jukumu la kuwalea
aliachiwa mama yao.
Alifafanua kuwa baba huyo ambaye wakati wa uhai wake alifahamika kwa
jina maarufu la ‘Moja kwa moja’, alikufa baada ya kuanguka kutoka juu ya
mti alipokuwa akirina asali na tangu hapo, jukumu la kulea likabaki kwa
mama mzazi wa watoto hao.
“Tukio hilo limetusikitisha sana ni tukio baya maana wameteketea
kabisa hajulikani nani ni nani,” alisema Sauli na kuongeza, “Hata Ester
hafahamiki alipo, kuna watu wengi lakini tumemuangalia hapa msibani
hatumuoni.”
Taarifa nyingine kutoka eneo la tukio, zilidai kuwa Mdachi alizaa na
mama huyo watoto wawili na baada ya kufariki, mama huyo alizaa watoto
wengine wawili na wanaume wengine.
Ajali barabarani Katika tukio lingine, ajali nyingine imetokea eneo
la mlima Sekenke wilayani Iramba kwenye barabara kuu ya Singida – Nzega
na kusababisha vifo vya watu wanne papo hapo na majeruhi wawili.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, Thobias Sedoyeka aliwataja
waliokufa katika ajali hiyo kuwa ni dereva wa gari hilo Thabit Ally na
abiria, Christopher Kilindiro (30) na Rajabu Shabani (25) ambao ni
wafanyabiashara na wakazi wa Igunga mkoani Tabora na mwanamume mmoja
ambaye jina lake halijapatikana.
Kwa mujibu wa Sedoyeka, waliojeruhiwa ni Lausius Charles Haule (15)
mwanafunzi wa darasa la saba shule ya msingi Igunga na Marwa Charles
(37) mfanyabiashara na mkazi wa Igunga na wamelazwa katika hospitali ya
Kiomboi wilayani Iramba kwa matibabu.
Kamanda Sedoyeka amesema kuwa ajali hiyo ilitokea juzi majira ya saa
3.00 asubuhi katika kijiji cha Misigiri na kuhusisha gari la mizigo
lenye usajili namba T.716 MMI na trela T. 391 DCY aina ya Scania mali ya
Hascam Investment & General Supplies Ltd ya jijini Dar es Salaam.
Alisema gari hiyo likisafiri kutoka Moshi kwenda Mwanza, huku likiwa
limepakia shehena ya mbolea liliacha njia na kutumbukia darajani na
kusababisha vifo vya watu hao wanne na majeruhi wawili.
Alisema uchunguzi wa awali wa chanzo cha ajali hiyo, umebaini kuwa breki za gari hilo zilishindwa kufanya kazi yake ipasavyo.
Imeandikwa na Sifa Lubasi, Dodoma na Abby Nkungu, Singida.
Chanzo Na Habari leo
0 comments:
Post a Comment