Home » » Wanufaika wa Mikopo ya Elimu Juu watakiwa kurejesha mikopo waliyopewa.

Wanufaika wa Mikopo ya Elimu Juu watakiwa kurejesha mikopo waliyopewa.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma


Wanufaika wa Mikopo ya Elimu ya Juu ambao tayari wapo katika ajira wametakiwa kurejesha marejesho ya mikopo waliyopewa kutokana na mfuko wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) kutegemea fedha hizo kuendelea kuwakopesha wanafunzi wengine.

Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa ameyasema hayo leo Bungeni, Mjini Dodoma alipokuwa akiwasilisha hotuba ya kuhitimisha mkutano wa tatu wa Bunge la kumi na moja.

“Uwezo wa Bodi ya mikopo ya Elimu ya Juu kuwahudumia walengwa unajengwa na fedha zinazotengwa kila mwaka katika mipango na Bajeti pamoja na marejesho ya mikopo iliyoiva kutoka kwa wanufaika,” alisisitiza Mhe. Majaliwa.

Aliendelea  kusema kuwa Serikali inaendelea kufanya maboresho ya kimfumo na kisheria ili kuimarisha urejeshwaji wa mikopo. Aidha amewaagiza waajiri wote Nchini kutekeleza wajibu wao wa kuingiza makato ya marejesho wa mikopo ya wanufaika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa baada ya kuwasiliana na Bodi ya Mikopo.

Vile vile Mhe. Majaliwa amesema kuwa Serikali inaendelea kuimarisha mfumo wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu sambamba na kushughulikia changamoto mbalimbali zilizopo katika Bodi ya mikopo ili kuhakikisha utoaji wa mikopo unafanyika kwa ufanisi.

Pia Serikali inategemea kubadilisha utaratibu wa kutoa mikopo ili kuwafikia wanafunzi wote wenye uhitaji zaidi wakiwemo yatima na wenye uwezo mdogo kiuchumi bila kujali aina gani ya program wanazozisomea.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Dodoma Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa