Lilian Lundo – MAELEZO – Dodoma
Wanufaika
wa Mikopo ya Elimu ya Juu ambao tayari wapo katika ajira wametakiwa
kurejesha marejesho ya mikopo waliyopewa kutokana na mfuko wa Bodi ya
Mikopo ya Elimu ya Juu (HESLB) kutegemea fedha hizo kuendelea
kuwakopesha wanafunzi wengine.
Waziri
Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa ameyasema hayo leo Bungeni, Mjini Dodoma
alipokuwa akiwasilisha hotuba ya kuhitimisha mkutano wa tatu wa Bunge la
kumi na moja.
“Uwezo
wa Bodi ya mikopo ya Elimu ya Juu kuwahudumia walengwa unajengwa na
fedha zinazotengwa kila mwaka katika mipango na Bajeti pamoja na
marejesho ya mikopo iliyoiva kutoka kwa wanufaika,” alisisitiza Mhe.
Majaliwa.
Aliendelea kusema
kuwa Serikali inaendelea kufanya maboresho ya kimfumo na kisheria ili
kuimarisha urejeshwaji wa mikopo. Aidha amewaagiza waajiri wote Nchini
kutekeleza wajibu wao wa kuingiza makato ya marejesho wa mikopo ya
wanufaika kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa baada ya kuwasiliana
na Bodi ya Mikopo.
Vile
vile Mhe. Majaliwa amesema kuwa Serikali inaendelea kuimarisha mfumo wa
utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu sambamba na
kushughulikia changamoto mbalimbali zilizopo katika Bodi ya mikopo ili
kuhakikisha utoaji wa mikopo unafanyika kwa ufanisi.
Pia
Serikali inategemea kubadilisha utaratibu wa kutoa mikopo ili kuwafikia
wanafunzi wote wenye uhitaji zaidi wakiwemo yatima na wenye uwezo mdogo
kiuchumi bila kujali aina gani ya program wanazozisomea.
0 comments:
Post a Comment