Na: Immaculate Makilika- Dodoma
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli amewaasa watanzania kudumisha
amani iliyopo ambayo ilipatikana baada ya Mashujaa mbalimbali kuipigania na
hata kujitoa uhai wao kwa ajili ya Taifa.
Akizungumza leo, wakati akihutubia
wananchi mara baada ya kumaliza shughuli za maadhimisho ya Siku ya kumbukumbu
ya Mashujaa iliyofanyika katika viwanja vya Mashujaa vilivyopo mjini
Dodoma.
Rais Magufuli alisema kuwa
maadhimisho ya kumbukumbu za Mashujaa ni muhimu kwa vile watu hao
walijotoa kwa ajili ya kulitetea taifa.
“Wakati tunawakumbuka waliotangulia
mbele za haki, sisi tuliobaki tudumishe amani hii, kama ambavyo wao
waliotutangulia hawakujali dini zao bali taifa hili” alisema Rais Magufuli.
Aliongeza kuwa nchi ya Tanzania
imebaki kuwa kisiwa cha amani, na amani hiyo isichezwe bali ijengwe na
kudumishwa kwa umoja na mshikimamano ili kusaidia kuitangaza nchi zaidi.
Aidha, viongozi mbalimbali wa Serikali
akiwemo Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Mheshimiwa Dkt.Ali Mohamedi
Shein, Rais Mstaafu wa Awamu ya Pili Mheshimiwa Alhaji Ali Hassan Mwinyi,
Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa John Samweli Malecela nao wapewa fursa ya
kuzungumza na wananchi kuhusu maadhimisho hayo ya kumbukumbu ya siku ya
Mashujaa.
Viongozi hao, wamesisitiza umuhimu wa
kudumisha amani iliyopo na kusema kuwa ni jukumu la wananchi wote
kuhakikisha hawashiriki katika vitendo vitakavyosababisha
uvunjifu wa amani.
Ambapo, waliwataka wananchi kuwaombea
Mashujaa wote waliofariki katika vita mbalimbali wakiwa katika
harakati za kulifanya Taifa la Tanzania kuwa huru.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu
Mheshimiwa Kassim Majaliwa, alisema kuwa atahakikisha anasimamia utekelezaji wa
agizo la Rais la kuitaka Serikali kuhamia mjini Dodoma.
“Nahamia Dodoma mwezi wa tisa,na
nitakapohamia mawaziri wote lazima wanifuate. Katika hili nitasimamia kwa nguvu
zote” alisema Waziri Mkuu Majaliwa.
Awali, Mheshimiwa Rais Magufuli
alisema kuwa atahakikisha katika kipindi cha utawala wake, Serikali inahamia
mjini Dodoma, kwa vile Rais wa Awamu ya kwanza Mwl. Julius Nyerere alionesha
nia ya kufanya hivyo.
Aliongeza kuwa kwa
sasa mji wa Dodoma unaweza kukidhi mahitaji hayo ya Serikali kwa kutumia
miundombinu iliyopo, hata hivyo Serikali inaendelea kujenga miundombinu mipya.
Maadhimisho ya kumbukumbu za Mashujaa
hufanyika Julai 25, ya kila mwaka, kwa kufanya maombolezo ya
Mashujaa waliopigana katika vita mbalimbali katika harakati za kutetea uhuru wa
nchi ya Tanzania.
Maadhimisho ya mwaka huu
yamefanyika kwa mara ya kwanza mjini Dodoma, ambapo Rais John Pombe Magufuli
alikuwa mgeni rasmi, ikiwa ni mara yake ya kwanza kuhudhuria maadhimisho hayo
kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
mwisho
0 comments:
Post a Comment